Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
UEFA yapanga kubadili utaratibu wa penalti
Shirikisho la Soka barani Ulaya UEFA limesema linatathmini utaratibu wa kupigwa kwa mikwaju ya penalty baada ya mechi kuufanya uwe wa haki zaidi.
Shirikisho hilo tayari limeanza kufanyia majaribio utaratibu mpya.
Badala ya klabu kubadilishana mmoja baada ya mwingine, UEFA inatafakari uwezekano wa kufuata utaratibu sawa na unaofuatwa katika mchezo wa tenisi.
Utaratibu huo unafanyiwa majaribio katika michuano ya ubingwa wa Ulaya kwa wachezaji wa chini ya miaka 17 ambayo ilianza Croatia Jumatano.
Kwa sasa, baada ya atakayeanza kupiga penalti kuamuliwa kwa kurushwa kwa sarafu juu, baadaye huwa ni kupishana.
Mfano mchezaji wa timu A akianza, anafuata wa timu B kisha anarudi mchezaji wa timu A.
Utaratibu mpya unaitwa ABBA ambapo mchezaji wa timu A akianza, atafuatwa na wawili wa B kabla ya mchezaji wa A kupiga.
Sarafu bado itarushwa kuamua atakayeanza.
Pendekezo hilo linatokana na ugunduzi kwamba timu inayofuata kwa kupiga penalti wachezaji wake hukabiliwa na shinikizo zaidi, kwani kila mara huwafuata wapinzani.
Utafiti unaonesha kwenye matuta, klabu inayotangulia kupiga mkwaju imekuwa ikishindwa katika asilimia 60 ya michuano yote.