Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema timu ya Marekani inaelekea Pakistan kwa mazungumzo na Iran

Akionya kuwa hakutakuwa tena na “huruma” iwapo mazungumzo yatashindikana, Trump amesema madaraja na vituo hivyo vya umeme “vitaanguka haraka, na vitaanguka kwa urahisi.”

Moja kwa moja

Na Lizzy Masinga

  1. Polisi wanasema sumu ya panya imepatikana kwenye kopo la chakula cha watoto nchini Austria

    Polisi nchini Austria wamewataka watu kuwa waangalifu baada ya sampuli ya chakula cha watoto cha HiPP kugundulika kuwa na sumu ya panya.

    Polisi katika eneo la mashariki la Burgenland wamesema kopo hilo la chakula cha karoti na viazi liliripotiwa na mteja, na kwa bahati nzuri mtoto hakula chakula hicho.

    Polisi wanasema kopo hilo linaonekana kuwa lilichezewa au kufanyiwa uharibifu. Mamlaka zinaamini kuwa kuna kopo jingine lenye sumu bado lipo sokoni, na zimetoa maelekezo ya jinsi ya kutambua makopo yenye dosari.

    Hata hivyo, taarifa ya polisi imesema onyo hilo lilitoka kwa wachunguzi wa Ujerumani, na makopo yaliyo na dosari pia yamekamatwa katika Jamhuri ya Czech na Slovakia.

    Siku ya Jumamosi, kampuni ya HiPP ilirejesha aina zote za chakula cha watoto cha kwenye makopo kinachouzwa katika maduka ya Spar nchini Austria, ikisema kula chakula hicho kunaweza kuwa hatari kwa maisha.

    Kampuni hiyo yenye makao yake Ujerumani imesema kurejeshwa kwa bidhaa hizo si kwa sababu ya tatizo la ubora au uzalishaji, na kwamba makopo yalitoka kiwandani yakiwa katika hali nzuri kabisa.

    Imeongeza kuwa tukio hilo linahusiana na kitendo cha uhalifu kinachochunguzwa na mamlaka.

  2. Vifo vimeripotiwa nchini Lebanon mwishoni mwa wiki licha ya kuwepo kwa usitishaji wa mapigano

    Makubaliano ya kusitisha mapigano kati ya Marekani na Iran, pamoja na yale kati ya Israel na Lebanon, yanaonekana bado yanaendelea kutekelezwa, lakini kumekuwa na matukio kadhaa yaliyoripotiwa ambayo yamesababisha vifo.

    Kusini mwa Lebanon, Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF) limesema wanajeshi wawili wamefariki dunia tangu makubaliano ya kusitisha mapigano yaanze kutekelezwa.

    Vyombo vya habari vya Israel vinaripoti kuwa Sajenti Barak Kalfon alikufa katika mlipuko alipokuwa akisafisha majengo siku ya Ijumaa, ambapo pia wanajeshi wengine watatu walijeruhiwa.

    Sajenti Lidor Porat aliuawa katika tukio jingine lililosababisha watu wengine tisa kujeruhiwa, jeshi la Israel limetangaza leo.

    Vyombo vya habari vya ndani vinasema gari la kivita walilokuwa wakisafiria wanajeshi hao liligonga bomu la ardhini, na Israel itachunguza kubaini bomu hilo liliwekwa lini, ikiwa ni ukiukwaji wa makubaliano ya kusitisha mapigano.

    Kwa upande mwingine, mwanajeshi wa kulinda amani kutoka Ufaransa anayehudumu katika Kikosi cha Mpito cha Umoja wa Mataifa nchini Lebanon (UNIFIL) pia aliuawa katika shambulio linalodaiwa kutekelezwa na Hezbollah.

    Kundi hilo lenye uungwaji mkono wa Iran limekanusha kuhusika na tukio hilo.

    Unaweza kusoma;

  3. Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema timu ya Marekani inaelekea Pakistan kwa mazungumzo na Iran

    Rais wa Marekani, Donald Trump amesema “Wawakilishi wangu wanaelekea Islamabad, Pakistan, watakuwa huko kesho jioni kwa ajili ya mazungumzo,” ameandika kwenye mitandao ya kijamii.

    “Tunatoa makubaliano ya haki na ya busara sana, na ninatumaini watayakubali kwa sababu wasipofanya hivyo, Marekani itaangamiza kila kituo cha umeme na kila daraja nchini Iran,” ameongeza.

    Akionya kuwa hakutakuwa tena na “huruma” iwapo mazungumzo yatashindikana, Trump amesema madaraja na vituo hivyo vya umeme “vitaanguka haraka, na vitaanguka kwa urahisi.”

  4. Hakuna dalili ya meli kupita katika Mlango-Bahari wa Hormuz

    Kama tulivyoripoti, Iran imefunga tena Mlango-Bahari wa Hormuz ikiwa ni hatua ya kujibu kuendelea kwa zuio la Marekani dhidi ya bandari zake.

    Tovuti ya kufuatilia meli ya MarineTraffic inaonyesha kuwa kwa sasa hakuna meli zinazovuka njia hiyo muhimu, ingawa nyingi zinaonekana zimetia nanga katika Ghuba, haswa karibu na pwani za Oman na UAE.

    Baadhi ya meli zilipita katika njia hiyo jana, lakini shughuli zilipungua kwa kasi baada ya Tehran kutangaza kufungwa kwa njia hiyo ya majini.

    Aidha, meli kadhaa zimeripoti kushambuliwa kwa makombora, huku meli moja ya mafuta ikisema ililengwa na mashambulizi kutoka kwa boti za kijeshi za Iran siku ya Jumamosi.

    Unaweza kusoma;

  5. Iran yasema vikwazo vya Marekani ni 'ukiukaji wa masharti ya kusitisha mapigano'

    Jeshi la majini la Iran lilisema kwamba kuendelea kwa vikwazo vya Marekani kwenye bandari za Iran ni "ukiukaji wa masharti ya kusitisha mapigano".

    Mapema mwezi huu Iran na Marekani zilikubaliana kusitisha mapigano kwa masharti ya wiki mbili, ambapo walikubaliana kwamba Meli zitaruhusiwa kupitia Mlango-Bahari wa Hormuz.

    Njia muhimu ya meli imefungwa tena na Iran na jeshi la majini la Iran linasema itaendelea kufungwa hadi kizuizi cha meli na bandari za Iran kitakapoondolewa.

    Katika taarifa yake ya hivi karibuni, Jeshi la Iran linasema taarifa zilizotolewa na Trump kwenye Mlango-Bahari wa Hormuz "hazina uhalali wowote".

    Haijulikani wazi ikiwa taarifa hiyo inarejelea maoni maalum yaliyotolewa na rais wa Marekani.

    Trump aliwaambia waandishi wa habari katika Ofisi ya Oval Jumamosi kwamba viongozi wa Iran wanataka kufunga mlango-bahari, lakini Marekani haitawaruhusu "kututishia".

    Unaweza kusoma;

  6. Papa asema hotuba ya 'madhalimu' haikuwa ikimlenga Trump

    Papa Leo amesema hakutaka kujibizana na Donald Trump alipokosoa “madikteta” wanaotumia mabilioni ya dola kwenye vita katika hotuba aliyotoa mapema wiki hii.

    Papa huyo amesema maneno yake yaliandikwa wiki mbili kabla, “kabla kabisa ya rais kutoa maoni yoyote kunihusu.”

    Amesema haikuwa nia yake kuingia kwenye mjadala na rais huyo, jambo ambalo hapendezwi nalo.

    Donald Trump hapo awali alimshambulia Papa huyo wa kwanza kutoka Marekani, akisema ni “mbaya kwa sera za nje,” hasa baada ya Papa kukosoa operesheni ya kijeshi ya Marekani na Israel dhidi ya Iran.

    Papa huyo, ambaye yuko kwenye ziara barani Afrika, amesema kumekuwa na “simulizi isiyo sahihi” iliyojengwa kutokana na kauli za kisiasa za Trump.

    Makamu wa Rais wa Marekani JD Vance amesema anamshukuru Papa kwa ufafanuzi huo na akaongeza kuwa, ingawa mara nyingine kuna tofauti za maoni, hali halisi mara nyingi huwa ngumu zaidi kuliko inavyoonekana kwenye vyombo vya habari.

    Awali, kabla ya hotuba ya Papa kuhusu “madikteta,” Vance alikuwa ameshauri Vatican ijikite zaidi kwenye masuala ya maadili.

    Wakati wa hotuba yake nchini Cameroon siku ya Alhamisi, Papa aliwakosoa viongozi ambao "hupuuza ukweli kwamba mabilioni ya dola hutumika kwa mauaji na uharibifu, lakini rasilimali zinazohitajika kwa ajili ya uponyaji, elimu hazipatikani popote".

    "Mabwana wa vita hujifanya hawajui kwamba inachukua muda mfupi tu kuharibu, lakini mara nyingi maisha yote hayatoshi kujenga upya," alisema.

    Papa pia alilaani "mzunguko usio na mwisho wa uvunjifu wa utulivu na vifo" katika eneo "lenye damu" la Cameroon ambalo lilikuwa limekumbwa na uasi kwa karibu muongo mmoja.

    Maneno hayo yalitafsiriwa na baadhi kama marejeleo ya Trump - ambaye baadaye aliwaambia waandishi wa habari: "Papa anaweza kusema anachotaka, na mimi nataka aseme anachotaka, lakini siwezi kukubaliana naye."

    Unaweza kusoma;

  7. Marekani imesema nini kuhusu kuzuia bandari za Iran?

    Kizuizi cha majini cha Marekani dhidi ya meli zinazoingia na kutoka bandari za Iran kimekuwa kikiendelea wikendi hii.

    Donald Trump alitangaza kizuizi hicho wiki moja iliyopita, chini ya siku moja baada ya mazungumzo marefu kati ya Marekani na Iran nchini Pakistan kushindwa kufikia makubaliano.

    Vikosi vya Marekani vilisema vitazuia au kuzirudisha meli zinazosafiri kwenda au kutoka pwani ya Iran, bila kujali utaifa.

    Marekani inatarajia kuweka shinikizo kwa Iran kwa kupunguza uwezo wake wa kufaidika na mauzo ya mafuta nje ya nchi.

    Kamanda Mkuu wa Marekani alisema wikendi hii kwamba amelazimisha meli 23 kugeuka karibu na Mlango Bahari wa Hormuz tangu kizuizi hicho kilipoanza.

    Katika chapisho la mitandao ya kijamii lililochapishwa saa moja tu iliyopita, Centcom inasema "kizuizi hicho kimesimamisha kabisa biashara ya kiuchumi inayoingia na kutoka Iran kwa njia ya bahari".

    Hata hivyo, BBC Verify ilifuatilia takribani meli nne kutoka bandari za Iran ambazo zilionekana kuvuka mstari wa kizuizi cha Marekani.

    Unaweza kusoma;

  8. Iran yasema iko mbali na makubaliano ya amani na Marekani, huku mlango bahari wa Hormuz ukifungwa tena

    Spika wa bunge la Iran, Mohammad Bagher Ghalibaf, anasema kwamba ingawa "maendeleo yamepatikana" katika mazungumzo ya kukomesha vita na Marekani, pande hizo mbili "hazijakaribia kufikia makubaliano ya mwisho".

    Ghalibaf alikuwa Pakistani wiki iliyopita kwa mazungumzo ya amani na wajumbe wa Marekani, akiwemo Makamu wa Rais JD Vance.

    Hakuna tarehe iliyowekwa kwa ajili ya duru inayofuata ya mazungumzo.

    Unaweza kusoma;

  9. Habari za asubuhi, karibu katika taarifa zetu hii leo