Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Mlango bahari wa Hormuz uko wazi kwa meli za kibiashara, yasema Iran

Waziri wa mambo ya kigeni wa Iran, Abbas Araghchi ametangaza kuwa mlango bahari wa Hormuz uko wazi kwa muda ulio salia wa usitishaji mapigano

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Mariam Mjahid & Beldeen Waliaula

  1. Mtoto wa Mugabe akiri kosa la kumnyooshea mtu bunduki Afrika Kusini

    Mtoto wa rais wa zamani wa Zimbabwe, Robert Mugabe amekiri kosa la kumtishia mtu na bunduki na kuwa nchini Afrika Kusini kinyume cha sheria.

    Bellarmine Mugabe amekubali mashtaka hayo mawili baada ya kukamatwa mwezi Februari kufuatia tukio la kumpiga risasi kijana wa miaka 23 nyumbani kwake mjini Johannesburg.

    Kijana huyo mwenye umri wa miaka 28 amekuwa akizuiliwa pamoja na mtuhumiwa mwenza Tobias Matonhodze, na amefikishwa mahakamani mjini Alexandra hii leo.

    Mawakili wa wawili hao waliiambia mahakama kuwa wateja wao, wako tayari kurejea nchini kwao Zimbabwe kwa gharama zao wenyewe ikiwa hawatapewa adhabu ya kifungo.

    Matonhodze, mwenye umri wa miaka 33, alikiri pia mashtaka ya jaribio la kutekeleza mauaji, kuzuia haki kutendeka, kuingia nchini Afrika Kusini kinyume cha sheria na kumiliki risasi.

    Bellarmine Mugabe, ambaye pia awali alishtakiwa kwa jaribio la mauaji, alizungumza tu kuthibitisha kuwa anaelewa mashtaka yanayomkabili na atakubali mashtaka baada ya kuafikia makubaliano na waendesha mashtaka.

    Wawili hao walikamatwa tarehe 19 mwezi Februari baada ya polisi kuitwa nyumbani kwa Mugabe katika eneo la kifahari la Hyde Park mjini Johannesburg.

    Mwanaume anayeaminika kuwa mlinzi wa lango, alipelekwa hospitalini akiwa hali mahututi baada ya kupigwa risasi.

    Hukumu ya kesi hiyo inatarajiwa kutolewa tarehe 24, mwezi Aprili.

    Pia unaweza kusoma:

  2. Kizuizi cha kijeshi cha Marekani kitaendelea - Trump

    Rais wa Marekani Donald Trump amechapisha ujumbe kwenye mtandao wa Truth Social na kurejelea kuwa “mlango bahari wa Hormuz uko wazi na tayari kwa biashara”

    Hata hivyo ameongeza kuwa:

    “Lakini kizuizi cha kijeshi kitaendelea kutekelezwa kwa nguvu zote, hadi pale tutaafikiana na Iran kwa 100%”

    Rais huyo pia amesema kuwa mchakato huo unatarajiwa kufanyika haraka kwa kuwa sehemu kubwa ya masuala tata tayari yamejadiliwa.

    “Mchakato huu unapaswa kwenda haraka sana kwa kuwa sehemu kubwa ya vipengele vya mkataba wa makubaliano yameafikiwa. Asanteni kwa kuzingatia jambo hili” alisema Trump.

    Pia unaweza kusoma:

  3. Mlango bahari wa Hormuz uko wazi, asema waziri wa mambo ya kigeni wa Iran

    Mlango bahari wa Hormuz uko wazi kwa muda wa usitishwaji mapigano uliosalia, amesema Waziri wa mambo ya kigeni wa Iran, Abbas Araghchi.

    Katika taarifa aliyochapisha kwenye mtandao wa X, Waziri huyo aliandika kuwa, “Kulingana na usitishwaji wa mapigano nchini Lebanon, njia ya kupita kwa meli zote za kibiashara(mlango bahari wa Hormuz) uko wazi kwa kipindi kilichosalia cha usitishwaji mapigano, kwa njia zilizoratibiwa kama ilivyotangazwa na Shirika la Bandari na Usafiri wa Baharini la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.”

    Mapema wiki hii Marekani ilikuwa imetangaza kuwa imeanza kutekeleza kizuizi cha kijeshi katika bandari za Iran na mlango bahari wa Hormuz.

    Trump alitangaza usitishwaji wa mapigano nchini Iran kwa muda wa wiki mbili ili kutoa nafasi kwa mazungumzo ya amani kufanyika. Muda wa usitishwaji huo unakamilika tarehe 22 mwezi Aprili.

    Pia unaweza kusoma:

  4. "Hatutasalimisha silaha zetu" - Hezbollah

    Mmoja wa viongozi wakuu wa kundi la Hezbollah, Wafiq Safa, ameiambia BBC kuwa “hawatasalimisha silaha zao” hii ilikuwa saa chache tu kabla ya makubaliano ya kusitisha mapigano kati ya Israel na Lebanon kuanza kutekelezwa.

    Waziri mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, amekukuwa akisisitiza kuwa kuwapokonya silaha kundi hilo ni muhimu kabla ya kuendelea kufanya mazungumzo na serikali ya Lebanon.

    Alipoulizwa kuhusu suala la kusalimisha silaha, Safa alisema: “Haitawezekana hadi kuwe na usitishaji mapigano ya kweli. Hadi Israel iondoke Lebanon. Hadi pale ambapo wafungwa watarejea, waliokimbia makazi yao warejee na ujenzi wa nchi kuanza upya ,hatuwezi kuzungumzia silaha za Hezbollah.”

    Mahojiano hayo yaliyofanyika katika jengo la makazi mjini Beirut yanatoa mwanga kuhusu uratibu uliopo kati ya Hezbollah na mshirika wake mkuu wa kikanda, Iran.

    “Hezbollah na Iran ni kama roho mbili katika mwili mmoja,” Safa alisema. “Hezbollah haiwezi kuwepo bila Iran, wala Iran haiwezi kuwepo bila Hezbollah,” alielezea kuwa uhusiano huo ni wa “kidini, kisheria na kiitikadi.”

    Hezbollah, kundi la kisiasa na kijeshi la Waislamu wa Kishia, linapinga kuwepo kwa Israel na linatambuliwa kama shirika la kigaidi na Marekani, Uingereza, Israel na mataifa mengine.

    Kundi hilo lilijiunga na mzozo wa Marekani na Israel dhidi ya Iran kwa kurusha makombora kuelekea Israel mapema mwezi Machi, likisema lilikuwa likijibu mauaji ya kiongozi mkuu wa Iran na mashambulizi ya karibu ya kila siku ya Israel nchini Lebanon.

    Israel ilijibu kwa mashambulizi makali ya anga na uvamizi wa ardhini kusini mwa Lebanon, likisema litaendeleza kampeni yake hadi Hezbollah itakapo pokonywa silaha.

    Alipoulizwa kama Hezbollah inatanguliza maslahi ya watu wa Lebanon au ya Iran, Safa alisema “Bila shaka, Hezbollah inaangazia maslahi ya Lebanon.”

    Pia unaweza kusoma:

  5. Mashambulizi ya Israel yawauwa watu 13, kabla usitishwaji mapigano kuanza kutekelezwa

    Majeshi ya Israel yalishambulia mji wa Tyre nchini Lebanon usiku uliopita, na kuwaua watu 13 na kuwajeruhi wengine 35, kulingana na shirika la habari la taifa hilo, National News Agency.

    Mapema asubuhi ya leo, timu za uokoaji bado zilikuwa zikiendelea kuwatafuta watu 15 ambao wanaaminika kukwama kwenye vifusi.

    Mashambulizi hayo yalitokea muda mfupi kabla ya usitishaji wa mapigano wa siku 10 kati ya Israel na Lebanon kuanza kutekelezwa rasmi.

    Pia unaweza kusoma:

  6. "Nitafanya kila tuwezalo kuhakikisha mlango bahari wa Hormuz unasalia wazi" - Keir Starmer

    Waziri mkuu wa Uingereza ambaye yuko ziarani nchini Ufaransa, amesema kuwa “tutafanya kila tuwezalo” kupunguza athari za kufungwa kwa mlango bahari wa Hormuz.

    Starmer alisema kuwa “ni muhimu kuunda muungano wa mataifa utakaokuwa na msimamo kuwa makubaliano ya kusitisha mapigano lazima yadumu, iwapo yataafikiwa na mlango wa Hormuz usalie wazi”

    “Suala hili linahusu maslahi yetu sote, kwa sababu kinachoendelea nchini Iran kinaathiri uchumi wa kila mmoja wetu. Ndio maana mataifa yanakuja pamoja.”

    “Kila mtu anaelewa kuwa ili kufanikisha hilo, tunahitaji mkakati wa kidiplomasia na kisiasa, tunahitaji mkakati wa utaratibu na kiuchumi, na pia tunahitaji mipango ya kijeshi na hayo ndiyo tunayo yajadili leo.”

    Keir Starmer na Emmanuel Macron wa Ufaransa wanaongoza mkutano kwa njia ya mtandao unaoshirikisha takriban mataifa 40, unaolenga kuanzisha operesheni ya kimataifa ya kuhakikisha usalama wa meli zinazopita mlango bahari wa Hormuz.

    Pia unaweza kusoma:

  7. Masharti yepi yaliafikiwa katika makubaliano ya kusitisha mapigano kwa muda kati ya Israel na Lebanon ?

    Rais wa Marekani Donald Trump alitangaza kuwa viongozi wa Israel na Lebanon wamekubaliana kusitisha mapigano kwa siku 10 kuanzia tarehe 16 mwezi Aprili.

    Katika taarifa yake, Trump hakuijumuisha kundi la Hezbollah ambalo limekuwa likishambuliana na Israel kwa muda wa wiki sita.

    Ila baadaye Trump alitoa wito kwa kundi hilo kuheshimu makubaliano ya sasa ya kusitisha mapigano.

    Trump pia anataka kuwakutanisha Waziri mkuu wa Israel na Rais wa Lebanon katika ikulu ya White house

    Lakina kabla ya hilo, mkataba wa kusitisha mapigano kwa muda nchini Lebanon unasemaje?

    Makubaliano hayo yanasitisha mapigano kwa siku 10, na kuna uwezekano wa muda huo kuongezwa iwapo mazungumzo yanayoendelea yataonyesha mafanikio.

    Kulingana na mkataba huo;

    • Israel ina haki ya kuendelea kujilinda dhidi ya mashambulizi yoyote
    • Pande zote mbili zinatambua kuwa vikosi vya Lebanon pekee ndivyo vina jukumu la kulinda taifa hilo.
    • Lebanon inapaswa kuchukua hatua ya kuzuia Hezbollah na makundi mengine, kutofanya mashambulizi dhidi ya Israel
    • Israel na Lebanon wote waimeitaka Marekani kuendelea kusimamia mazungumzo hayo.

    Licha ya makubaliano hayo, Israel imesisitiza kuwa wanajeshi wake watasalia kusini mwa Lebanon.

    Pia unaweza kusoma:

  8. Hezbollah yasema iko "macho na tayari kwa mashambulizi" iwapo makubaliano ya kusitisha mapigano yatakiukwa

    Kundi la Hezbollah limesema linaendelea kuweka “kidole kwenye kitufe cha kufyatua risasi” iwapo kutatokea “usaliti” kutoka kwa Israel kipindi hiki cha usitishwaji mapigano nchini Lebanon.

    Katika taarifa, kundi hilo linaloungwa mkono na Iran limesema wametekeleza mashambulizi 2,184 dhidi ya Israel kuanzia tarehe 2 mwezi Machi hadi tarehe 16 mwezi Aprili.

    Baada ya taarifa ya Trump ya kusitishwa kwa mapigano kwa muda wa siku 10, Hezbollah imesema “usitishaji wowote wa mapigano lazima uwe wa jumla katika maeneo yote ya Lebanon na haipaswi kuipa Israel uhuru wowote wa kufanya operesheni.”

    Israel ilikubali kusitisha mapigano kwa muda wa siku 10, lakini Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu alisisitiza kuwa wanajeshi wa Israel wataendelea kubaki kusini mwa Lebanon kipindi hiki cha usitishwaji mapigano.

    Pia unaweza kusoma:

  9. Abiy Ahmed asema Ethiopia haitaendelea kukosa njia ya bahari

    Waziri mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed ameeleza kuwa eneo la Pembe ya Afrika halitaweza kufikia amani ya kudumu hadi Ethiopia ipate njia ya kufikia bahari, akisisitiza kuwa suala hilo linahitaji kuangaliwa kwa umakini na kila mwananchi pamoja na taasisi zinazojihusisha na maendeleo na usalama wa eneo hilo.

    “Yeyote anayefikiri Ethiopia itapoteza haki yake ya kupata njia ya bahari amekosea,” amesema Waziri Mkuu Abiy Ahmed.

    Katika mahojiano maalum na shirika la utangazaji la serikali ya Ethiopia, Ethiopian Broadcasting Corporation, yaliyogawanywa katika sehemu mbili, Abiy amesema ukosefu wa bandari ya bahari unaipunguzia Ethiopia ushindani katika sekta ya viwanda.

    "Jambo kubwa linalozuia Ethiopia kuwa nchi inayolisha raia wake, inajitegemea, na inaweza kushindana kimataifa ni ukosefu wa bandari." asema Abiy.

    Baada ya Iran kufunga Mlango Bahari wa Hormuz hivi karibuni, imekuwa na athari kwa nchi zote ulimwenguni.

    Soma zaidi:

  10. Iran yatoa tahadhari kwa meli zinazopitia mlango bahari wa baab al mandab

    Mashirika ya habari yaliyo karibu na Walinzi wa Mapinduzi wa Iran yameripoti taarifa kutoka kundi linalojiita “Warriors Without Borders”, ambalo limetoa “onyo” kuhusu kuongezeka kwa mivutano ya kijeshi katika Bab al-Mandab Strait.

    Kundi hilo limesema kuwa meli zitakazopita katika mlango huo wa bahari zinapaswa “kuwa makini kutoka pande zote sita” kuanzia leo Ijumaa.

    Onyo hilo linaonekana kuashiria kwa njia isiyo ya moja kwa moja kuongezeka kwa mvutano katika eneo hilo, na uwezekano wa Bab al-Mandab kuhusishwa moja kwa moja katika mzozo kati ya Iran na Marekani.

    Katika taarifa hiyo, inadaiwa kuwa mmoja wa makamanda wa muqawama alitoa ujumbe wa tahadhari takriban saa moja kabla ya toleo rasmi la onyo hilo kali na lisilo la kawaida, akisema kuwa kuanzia mchana wa Ijumaa, kila anayepanga kupita Bab al-Mandab anapaswa kuwa makini zaidi kuliko kawaida kutoka kila upande.

    Soma zaidi:

  11. Uingereza na Ufaransa wataongoza mjadala kuhusu Mlango Bahari wa Hormuz

    Uingereza na Ufaransa wanatarajiwa kufanya mkutano na washirika wao baadaye leo kujadili juhudi za pamoja za kurejesha uhuru wa usafiri katika Mlango bahari wa Hormuz.

    Tehran imeathiriwa na hatua ya kufunga kwa njia hiyo muhimu ya baharini karibu na pwani ya Iran kufuatia mashambulizi ya Marekani na Israel, huku Marekani pia ikianza zuio lake dhidi ya bandari za Iran, hatua ambazo zimesababisha kupanda kwa bei za nishati duniani.

    Takriban nchi 40 zinatarajiwa kushiriki katika mkutano huo wa mchana huu, ofisi ya Waziri Mkuu Keir Starmer imesema, ikiongeza kuwa viongozi watajikita katika kuunga mkono usitishaji vita ulio dhaifu katika eneo hilo na kuhakikisha njia za usafirishaji zinafunguliwa na kulindwa kwa muda mrefu kupitia mlango huo wa bahari.

    Starmer anatarajiwa kuuambia mkutano kuwa kufunguliwa upya bila masharti kwa mlango huo ni wajibu wa kimataifa, kulingana na taarifa ya Downing Street.

    Aidha, watajadili uwezekano wa kupelekwa kwa “kikosi cha kijeshi cha kimataifa chenye lengo la ulinzi pekee” ili kuhakikisha uhuru wa usafiri, kwa mujibu wa mwaliko uliotumwa na Ikulu ya Élysée Palace na ulioonekana na AFP.

    Soma zaidi:

  12. Akiba ya mafuta ya ndege Ulaya yatabiriwa kutosheleza kwa wiki sita pekee

    Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Nishati (IEA) amesema kuwa Ulaya ina akiba ya mafuta ya ndege inayotosha kwa takriban wiki sita pekee.

    Shirika hilo limesema katika ripoti yake ya wiki hii kuwa mahitaji ya biashara yatafikia kiwango cha juu mwezi Juni endapo Ulaya haitafanikiwa kuchukua nafasi ya angalau nusu ya uagizaji wake wa mafuta kutoka Mashariki ya Kati.

    Mlango Bahari wa Hormuz, njia muhimu ya usafirishaji wa mafuta ya ndege, umeathiriwa kwa zaidi ya wiki sita kutokana na hatua za Iran kujibu mashambulizi ya Marekani na Israel, hali iliyosababisha bei kupanda kwa kasi.

    Mkurugenzi Mtendaji wa IEA, Fatih Birol, ameiambia AP kuwa safari za ndege huenda zikafutwa iwapo upungufu wa mafuta utaendelea.

    Katika ripoti yake ya soko la mafuta, IEA imesema mafuta ya Ghuba ndio husambaza mafuta ya ndege katika masoko ya dunia. Pia imesema nchi nyingine kubwa zinazouza mafuta yaliyosafishwa kama Korea, India na China zinategemea sana mafuta ghafi kutoka Mashariki ya Kati.

    Shirika hilo limesema hali hiyo imevuruga kwa kiasi kikubwa mfumo wa usambazaji wa mafuta ya anga.

    Hapo awali, Ulaya ilitegemea Mashariki ya Kati kwa hadi asilimia 75 ya uagizaji wake wa mafuta. Kwa sasa, nchi za Ulaya zinatafuta wauzaji mbadala kama Marekani na Nigeria.

    Amaar Khan, mkuu wa bei ya mafuta ya ndege ya Ulaya katika Argus Media, anaamini kwamba hata kama usambazaji kutoka Ghuba ukirejea hivi karibuni, bado huenda kukawa na upungufu katika wiki za mwanzo za msimu wa joto.

    "Sio uhakika, lakini bado, inaonekana kuna uwezekano mkubwa sana kwamba kutakuwa na uhaba kwa kiasi fulani katika baadhi ya maeneo ya Ulaya."

    "Bila shaka, eneo kama Heathrow linaweza kupewa kipaumbele kuliko viwanja vingine vidogo vya ndege, au vituo vilivyo na mahitaji kidogo. Lakini ndiyo, hata kama usambazaji huo utakuja, itachukua wiki tano hadi sita," alisema.

    Mashirika ya ndege duniani yamechukua hatua za haraka kukabiliana na kupanda kwa gharama za mafuta, ambayo kwa kawaida huchangia asilimia 20 hadi 40 ya gharama za uendeshaji.

    Soma zaidi:

  13. Pakistan yaanza kujiandaa kwa duru ya pili ya mazungumzo kati ya Marekani na Iran

    Wakati huo huo, polisi katika mji mkuu wa Pakistan, Islamabad, tayari wameanza maandalizi ya uwezekano wa ziara ya ujumbe wa kigeni, ingawa duru ya pili ya mazungumzo bado haijathibitishwa rasmi.

    Idara ya usimamizi wa trafiki ya jiji hilo imetangaza kufunga vituo vyote vya usafiri mjini Islamabad na katika mji jirani wa Rawalpindi kwa muda wa siku 10, kuanzia saa 11 jioni leo hadi Aprili 26.

    Huduma za usafiri wa umma kati ya Rawalpindi, Islamabad na maeneo mengine zitasitishwa. Aidha, polisi wa usafiri wa Islamabad wamepiga marufuku magari makubwa kuingia mjini kuanzia Aprili 18.

    Awali leo, Wizara ya Mambo ya Nje ya Pakistan ilisema kuwa hakuna tangazo rasmi kuhusu duru ya pili ya mazungumzo.

    Soma zaidi:

  14. Meli nne zinazohusiana na Iran zimevuka mstari wa zuio la Marekani

    Meli nne zimevuka mstari wa zuio la Marekani baada ya kuondoka katika bandari za Iran, kwa mujibu wa data za ufuatiliaji.

    Meli zote zilizofuatiliwa ni za kubeba makontena, tatu zikiwa zimebeba bendera ya Iran, na ya nne, Tava 4, ikiwa imesajiliwa nchini Comoro.

    Tangu zuio hilo lilipoanza saa 15:00 BST Jumatatu, meli zilizovuka na kufuatiliwa kupitia data ya trafiki ya majini ni:

    Azargoun — iliondoka bandari ya Shahid Rajee na kuvuka karibu saa 16:00, na inaelezwa kuwa ilielekea Kandla, kaskazini magharibi mwa India Ashkan3 — iliondoka bandari ya mashariki ya Iran ya Chabahar muda mfupi baada ya saa 12:00, na kwa sasa inaonekana ikiwa Karachi, Pakistan Shabdis — ambayo pia iliondoka Chabahar na kuvuka karibu saa 21:00, na inaonekana ikiwa karibu na pwani ya kusini magharibi mwa India, eneo la Kerala, ikielekea Zhuhai nchini China Tava 4 — iliondoka Bandar Imam Khomeini nchini Iran na kuvuka mstari wa zuio saa 13:00, na inaripotiwa kuwa karibu na pwani ya magharibi ya India ikielekea Bandari ya Jawaharlal Nehru karibu na Mumbai

    Tathmini hii inategemea nafasi zinazoripotiwa na meli kupitia mifumo yao ya ufuatiliaji. Hata hivyo, baadhi ya meli huenda zikazima vifaa vya ufuatiliaji au kutuma taarifa zisizo sahihi, mbinu inayojulikana kama “spoofing”.

    Katika mkutano na waandishi wa habari mapema leo, Jenerali Dan Caine alisema kuwa Marekani “inaendelea kudumisha zuio hilo”. Alipoulizwa kuhusu muda wa meli hizo kuvuka, Kamandi Kuu ya Jeshi la Marekani iliiambia BBC kuwa “haina cha kuongeza juu ya kauli za mwenyekiti huyo”.

    Soma zaidi:

  15. Vita vya Iran ‘vinapaswa kuisha hivi karibuni’- Trump

    Rais wa Marekani Donald Trump amesema ana matumaini kuwa kutafikiwa makubaliano ya amani na Iran akiongeza kuwa wako karibu mno kufikia makubaliano ya kuvimaliza vita.

    Rais Trump anasisitiza kuwa Iran imekubali kukabidhi madini yake ya urani ambayo yanaweza kutumika kutengeza silaha za kinyuklia.

    Kiongozi huyo wa Marekani amesema duru nyingine ya mazungumzo kati ya wajumbe wa nchi yake na wa Iran huenda ikafanyika Wikendi hii lakini ameonya kuwa huenda vita vikarejea iwapo hakutafikiwa makubaliano kati ya pande hizo mbili.

    Awali,Balozi wa Iran katika Umoja wa Mataifa amesema nchi yake iko katika hali ya ati ati kuhusu kufanyika kwa mazungumzo na Marekani.

    Soma zaidi:

  16. Usitishaji vita wa siku kumi kati ya Israel na Lebanon waanza kutekelezwa

    Makubaliano ya kusitisha mapigano kati ya Israel na Lebanon kwa siku kumi zijazo yameanza kutekelezwa.

    Makubaliano hayo yaliyosimamiwa na Marekani yanatarajiwa kurahisisha uwezekano wa mazungumzo ya kuvimaliza vita vya Iran.

    Kundi la wanamgambo linaloungwa mkono na Iran la Hezbollah limedokeza litayaheshimu makubaliano hayo.

    Saa chache tu baada ya kutangazwa kuwa makubaliano ya kusitisha mapigano yameanza kutekelezwa kati ya Lebanon na Israel, Jeshi la Lebanon limeripoti kuwa Israel imeyakiuka kwa kushambulia vijiji kadhaa vya kusini mwa nchi hiyo.

    Jeshi hilo limewatahadharisha wakaazi wa Kusini mwa Lebanon kutorejea makwao kwasababu hali bado ni tete.

    Israel imesisitiza kuwa Majeshi yake yatasalia katika maeneo inayoyadhibiti.

    Iran imesema imepokea vyema makubaliano hayo ya kusitisha vita lakini imetaka majeshi ya Israel kuondoka kabisa Lebanon.

    Zaidi ya watu 2,000 wameuawa katika mashambulizi hayo na zaidi ya watu milioni moja na laki mbili wameachwa bila ya makazi.

    Aidha Bwana Netanyahu amesema hajakubaliana na matakwa ya Hezbollah ya kuyaondoa majeshi yake kusini mwa Lebanon na kusisitiza kuwa kutasalia kile alichokitaja eneo salama mpakani na Lebanon na hadi mpaka wa Syria.

    Msemaji wa Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Steffane Dujarric amesema wamefurahishwa na hatua zilizochukuliwa na Israel na Lebanon kusitisha mapigano.

    Iwapo makubaliano hayo yatadumu basi huenda ikasafisha njia ya kufikiwa makubaliano ya amani kati ya Israel, Marekani na Iran na itakuwa ushindi mkubwa kwa utawala wa Trump ambao umekuwa ukipata tabu kukabiliana vilivyo na Iran hususan kuishinikiza kufungua Mlango Bahari wa Hormuz na kuachana na mpango wake wa Kinyuklia.

    Soma zaidi:

  17. Karibu kwa matangazo ya moja kwa moja.