Pakistan yataka Marekani na Iran kuheshimu usitishaji mapigano baada ya kushindwa kukubaliana
Wizara ya Mambo ya Nje ya Pakistan imetoa wito kwa Marekani na Iran kuendelea kuheshimu makubaliano ya muda ya kusitisha mapigano kufuatia mazungumzo ya amani yaliyofanyika Islamabad.
Katika taarifa iliyotolewa, Pakistan imesisitiza kuwa ni “muhimu sana” kwa pande zote mbili kuendelea kusimamia ahadi yao ya kusitisha mapigano, licha ya kushindwa kufikia makubaliano ya mazungumzo kuhusu mzozo wao.
Taarifa hiyo imeeleza matumaini kuwa Marekani na Iran wataendeleza mazungumzo kwa nia njema ili kufikia amani ya kudumu na ustawi si tu katika eneo la Mashariki ya Kati bali pia kimataifa.
Pakistan, ambayo imekuwa mpatanishi mkuu wa mazungumzo hayo, imesema itaendelea kuwezesha mazungumzo kati ya pande hizo mbili katika siku zijazo, ikilenga kusaidia kupunguza mvutano na kusaka suluhisho la kudumu.
Nchi hizo zilikaa kwa saa 21 usiku wa kuamkia leo kwa saa za Afrika Mashariki, lakini zilishindwa kufikia makubaliano ya kusitisha vita kutokana na kila upande kusema masharti ya mwezie hayakuwa yanakubalika.