Mazungumzo yaligubikwa na “kutoaminiana, mashaka na wasiwasi" - Iran

Chanzo cha picha, Getty Images
Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran imesema mazungumzo ya amani yaliyofanyika Islamabad, Pakistan, yalifanyika katika mazingira yaliyojaa mashaka, kutoaminiana na tahadhari kubwa kati ya pande zilizohusika.
Msemaji wa wizara hiyo, Esmaeil Baghaei, amesema haikutarajiwa kwamba Iran na Marekani zingefikia makubaliano ya haraka katika kikao kimoja tu cha mazungumzo.
Ameeleza kuwa kutokana na historia ya mvutano na kile alichokiita “vita vilivyowekwa kwa muda wa zaidi ya siku 40”, hali ya mazungumzo ilikuwa tayari imeathiriwa na ukosefu wa uaminifu kati ya pande hizo mbili.
Baghaei amesisitiza kuwa hakuna mtu aliyekuwa na matarajio ya kufikia makubaliano ya haraka, akibainisha kuwa mchakato wa mazungumzo ya aina hiyo huhitaji muda na hatua nyingi.
Hata hivyo, ameongeza kuwa diplomasia bado haijafungwa mlango wake, akisisitiza kuwa mazungumzo yanaweza kuendelea licha ya changamoto zilizopo.


