Lebanon ilidhani kulikuwa na usitishaji mapigano, Israel ikaanzisha mashambulizi makali

Muda wa kusoma: Dakika 5

Silaha zilipaswa kutulizwa.

Ilikuwa, baada ya yote, saa chache tu baada ya Rais wa Marekani Donald Trump kutangaza kwamba kusitishwa kwa mapigano kwa wiki mbili kulikubaliwa ili kusitisha vita katika Mashariki ya Kati.

Lakini wakati eneo hilo likianza kupata nafuu, ndege za kivita za Israel zilifanya mashambulizi ya dakika 10 kote nchini Lebanon, shambulio kubwa la anga lililoua takribani watu 203 na kuwajeruhi zaidi ya 1,000, kwa mujibu wa wizara ya afya ya Lebanon.

Ujumbe wa haraka wa kulaani kutoka kwa wakazi wa eneo hilo na nchi za Magharibi kulienea kwa kasi, lakini hakuna ukosoaji uliotolewa na Marekani dhidi ya mshirika wake katika vita hivi.

Iran ilisema kuwa huu ni "ukiukaji mkubwa" wa makubaliano ya kusitisha mapigano na imeiomba Marekani kusimamisha "uchokozi" wa Israel.

Maafisa wa Lebanon wanasema zaidi ya watu 1,700 wameuawa tangu Israel ilipoanza kampeni yake mpya nchini humo mwezi uliopita.

Israel imesema operesheni zake zinalenga kuidhoofisha Hezbollah na kufanikisha kile inachokiita malengo yake ya kijeshi yaliyosalia.

Vita vilianza na mashambulizi ya Marekani na Israel dhidi ya Iran tarehe 28 Februari, yakichochea kulipiza kisasi kutoka Tehran dhidi ya washirika wa Marekani katika Ghuba, na kutoka kwa vikundi vinavyoungwa mkono na Iran, Hezbollah nchini Lebanon na Houthi movement nchini Yemen dhidi ya Israel.

Kujibu hilo, Israel ilianza kushambulia Hezbollah na hata kuamuru wanajeshi wake kukalia sehemu kubwa za Lebanon.

Kusitishwa kwa mapigano kwa muda wa wiki mbili kulitangazwa na Waziri Mkuu wa Pakistan, Shehbaz Sharif, ambaye amekuwa akihudumu kama mpatanishi kati ya pande zinazopigana. Sharif alisema Marekani na washirika wake "wamekubaliana kusitisha mapigano mara moja kila mahali ikiwa ni pamoja na Lebanon na kwingineko."

Pakistan inatarajiwa kuandaa mazungumzo hayo Ijumaa, ambapo mpango wa vipengele 15 wa Marekani na mapendekezo ya vipengele 10 ya Iran yanaonekana kuwa msingi wa kuanzia kwa mazungumzo hayo.

Mpango wa Iran unasisitiza kusitishwa kwa mapigano katika pande zote, "ikiwa ni pamoja na dhidi ya upinzani wa Lebanon", akimaanisha mshirika wake wa Kishia nchini Lebanon.

Hata hivyo, serikali ya Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu ilisema kuwa makubaliano ya kusitisha mapigano hayahusishi Lebanon.

Donald Trump pia alisema Lebanon haikuwa sehemu ya makubaliano hayo "kwa sababu ya Hezbollah." Kwa mujibu wake, vita nchini Lebanon ni "mapigano tofauti."

Ilikuwa karibu saa 8:00 mchana mjini Beirut (saa 5:00 asubuhi GMT) wakati anga ya Lebanon lilipokumbwa na giza.

Vikosi vya Israel vilisema kuwa ndani ya dakika 10 ilikuwa "imekamilisha shambulio kubwa zaidi lililoratibiwa kote Lebanon tangu kuanza kwa Operesheni Roaring Lion", jina la operesheni ya Israel dhidi ya Iran.

Ilisema ililenga "makao makuu zaidi ya 100 ya Hezbollah, mifumo ya kijeshi, na vituo vya amri na udhibiti katika Beirut, Bonde la Bekaa na kusini mwa Lebanon."

Maeneo yenye watu wengi katikati ya Beirut yalishambuliwa katika mashambulizi yaliyoelezwa na maafisa kuwa miongoni mwa mashambulio makali zaidi tangu Hezbollah ilipojiunga na mzozo mapema Machi.

Sio tu ngome ya kawaida ya Hezbollah ya Dahieh iliyoshambuliwa katika mji mkuu wa Lebanon, pia katikati ya mji ililengwa.

Majeruhi waliripotiwa katika Bonde la Bekaa mashariki, pamoja na maeneo ya kusini ya Nabatieh, Sidon na Tyre.

Inaonekana Hezbollah ilikumbwa na mshangao, majibu yao pekee yalikuwa ni kurusha makombora kuelekea Israel saa chache baadaye.

Siku ya Alhamisi, Israel iliendelea na mashambulizi yake, ikisema kuwa imewaua "zaidi ya magaidi 70."

IDF pia ilisema kuwa "IMEWAANGAMIZA: Ali Yusuf Harshi, katibu binafsi wa Katibu Mkuu wa Hezbollah Naim Qassem mjini Beirut."

Hakuna uthibitisho uliotolewa. BBC haiwezi kuthibitisha madai hayo.

Asubuhi hiyo yenye upepo mtulivu na jua kali, kulikuwa na hali nzito mjini Beirut. Kwa kawaida mitaa huwa na msongamano wa magari, lakini nchi ilikuwa inasherehekea siku ya maombolezo ya kitaifa.

Waziri Mkuu Nawaf Salam alisema raia walilengwa, waliouawa na kujeruhiwa ni "mashahidi na waliojeruhiwa."

Rais Joseph Aoun alielezea tukio hilo kama "mauaji ya halaiki."

Katika baadhi ya maeneo, shughuli za utafutaji na uokoaji bado zinaendelea.

Hakuna kilichobaki cha jengo la ghorofa 10 la makazi lililoshambuliwa katika eneo la Tallet el Khayat, kitongoji cha watu wenye uwezo, magharibi mwa Beirut, mojawapo ya maeneo mengi yaliyoshambuliwa.

Shambulio la anga lilitokea bila onyo na liliwashangaza watu wote, kwani eneo hilo si miongoni mwa maeneo yaliyokuwa yakilengwa.

Vikosi vya ulinzi wa kiraia sasa vinaendelea kuchunguza majengo hapa na kote nchini, lakini kuna matumaini kidogo kwa watu ambao bado wana wapendwa wao waliopotea.

Ziad Samir Itani, ambaye alikuwa akiongoza timu ya ulinzi wa kiraia, alisema hili ni jambo "jipya kwa Beirut." Timu hizo zilikuwa zimechoka, baada ya zaidi ya wiki sita za mashambulizi ya mara kwa mara kutoka Israel.

"Nina uzoefu wa miaka 22. Kwa sisi, hili ni kama jambo la kawaida, lakini kwa watu wengine, si kawaida," Itani alisema, akiongeza, "Ninasikitika, kama kila mtu."

Ingawa Israel inasema iliilenga Hezbollah, ilijua kuwa hatua hiyo ingesababisha idadi kubwa ya vifo.

Ni vigumu kuona mkakati wa muda mrefu wa Israel ni upi. Hata maafisa wa kijeshi wa Israel wanakiri kile ambacho kimejulikana nchini Lebanon kwa muda mrefu: kwamba Hezbollah haiwezi kuvuliwa silaha kwa nguvu.

Mashambulizi hayo yanaweza kuipa Israel faida fulani ya kijeshi, lakini huenda ikawa ya muda mfupi na yenye mipaka.

Nchini Lebanon, wapinzani na wafuasi wa Hezbollah wanaungana kwa hasira, wakiwa na mtazamo mmoja kwamba kilichotokea hakikubaliki na hakina uhalali wowote.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Saeed Khatibzadeh, alikiambia kipindi cha Today cha BBC kwamba Marekani inapaswa kuchagua kati ya vita au amani.

Waziri huyo alisema Iran "itatoa usalama kwa usafiri " kupitia mlango bahari wa Hormuz, njia muhimu ya majini ambayo kufungwa kwake kumesababisha kupanda kwa bei ya mafuta na gesi,lakini kufunguliwa tena kutafanyika tu "baada ya Marekani kuondoa uchokozi huu," akimaanisha mashambulizi ya Israel nchini Lebanon.