Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Mambo 10 yatakayokusaidia kuwa tajiri
Jeff Bezos ni miongoni mwa watu matajiri zaidi duniani, huku utajiri wake ukikadiriwa kuwa kati ya dola bilioni 269 na dola bilioni 290.
Anaongoza moja ya kampuni zilizofanikiwa zaidi duniani, Amazon, ambayo yeye ni mmiliki wake.
Si kutia chumvi kusema kwamba kampuni hiyo ya teknolojia isingefanikiwa bila juhudi kubwa za Jeff Bezos.
"Kuibadilisha kampuni hii kutoka duka la bidhaa za vyakula hadi kuwa muuzaji wa kila aina ya bidhaa na huduma kunahitaji akili nyingi, ujasiri wa kuchukua hatari, mipango na ubunifu," alisema mwandishi wa habari David Baker, aliyeunda kipindi kinachoitwa "Inside the Mind of Jeff Bezos."
Maono ya Jeff Bezos hayakuhusu ujasiriamali pekee, bali pia mambo aliyoyathamini.
Lakini swali ni, Bezos alifanikiwaje kuifikisha kampuni hiyo katika kiwango hicho?
Hapa tunakuletea mambo 10 yaliyochangia mafanikio ya mmiliki wa Amazon, Jeff Bezos.
1. Kila tatizo lina suluhisho ukilitafakari na kutumia ubunifu
Bezos, tangu akiwa mtoto, aliamini katika nguvu ya ubunifu.
Wakati wa likizo za kiangazi, alitumia muda pamoja na babu yake, ambaye aliishi katika mji mdogo huko Texas. Katika kipindi hicho, alikuwa akitengeneza na kurekebisha vitu vilivyohitaji ujuzi wa ufundi na ubunifu.
Wakati mmoja, babu yake alipata kiasi kikubwa cha fedha kutokana na uvumbuzi wake wa vitu vya kisasa, baada ya kupata ajali ya gari na kupoteza kidole gumba. Alifanyiwa upasuaji na kutengenezewa kidole gumba bandia kwa kutumia mbinu ya kisasa.
Hii ni hadithi ambayo Bezos bado huisimulia hadi leo.
2. Mteja daima yuko sahihi
Tom Alberg, aliyekuwa mmoja wa viongozi wa Amazon, alimtaja Bezos kuwa "mtu mwenye kipaji cha asili katika kushughulika na wateja."
Aliongeza: "Anataka kubadilisha dunia, na mawazo yake daima yako kwenye kuridhisha wateja. Ukipata fedha, unaweza kufanya mambo mengi."
3. Jifunze kutokana na yaliyopita, kisha songa mbele
Sunil Gupta, profesa wa uchumi katika Chuo Kikuu cha Harvard, alielezea ubunifu wa Amazon kama kutengeneza bidhaa na huduma mpya kupitia kile alichokiita "kurudi nyuma kisha kupanua mbele."
Alimaanisha kuangalia nyuma na kuchunguza sababu zilizosababisha matatizo ya kampuni, kisha kutumia maarifa hayo kusonga mbele.
Hii ina maana kwamba Amazon huanza kwa kufikiria kile ambacho wateja wake wanataka, kisha hufanya kazi kuhakikisha wanakipata.
4. Kila siku ni siku ya kwanza
Kila ripoti ya mwaka inayotolewa na Amazon huambatanisha nakala ya barua ya kwanza ya kampuni kwa wanahisa wake.
Ujumbe huo unasisitiza umuhimu wa kuichukulia kila siku kama "siku ya kwanza" ya kampuni. Hii ina maana ya kuendelea kudumisha hamu ya ubunifu na mafanikio ya kibiashara.
Bezos amesisitiza mara kwa mara umuhimu wa mtazamo huo.
"Jambo muhimu ni kufikiria kwamba kampuni ndiyo imeanza siku hiyo na kwamba misingi yake ndiyo inawekwa," alisema.
5. Uwe jasiri kuliko wengi
Wakati matumizi ya intaneti yalipokuwa yakiongezeka kwa kasi mwaka 2000 na usalama wa kampuni ukiwa hatarini, Bezos alijitosa na kufungua Amazon kwa wawekezaji kutoka nje. Ilikuwa hatua kubwa ya ujasiri, na hatimaye ilizaa matunda.
Eneo moja ambalo hakufanikiwa sana ni biashara ya simu. Hata hivyo, imani ya Bezos katika usimamizi na kuchukua maamuzi magumu ni mkubwa.
Pia, si jambo geni kwake kuacha baadhi ya miradi na kuanzisha mingine akitumia mambo aliyojifunza kutokana na uzoefu wake.
John Rosman, aliyewahi kuwa mtendaji wa Amazon na mwandishi wa kitabu The Amazon Way, alisema Jeff Bezos "hana nia ya kufanya uamuzi bila kujua anakokwenda au jinsi atakavyofika huko," akitolea mfano teknolojia ya Alexa.
6. Kushindwa ni sehemu ya njia kuelekea mafanikio
Miradi ambayo haikufanikiwa haikuonyesha tu kiwango cha utayari wa Bezos kuhimiri vishindo, bali pia ilionyesha azma yake ya kuendelea hata baada ya kushindwa.
7. Usijutie kujaribu
Kutokuwa na hofu ya kushindwa kunamaanisha pia kutokujutia kujaribu.
Bezos alieleza wazi msimamo wake kuhusu jambo hilo wakati wa mazungumzo na Matthias Döpfner, Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya uchapishaji ya Axel Springer.
"Unapofikiria mambo ambayo utayajutia ukiwa na umri wa miaka 80, mara nyingi ni mambo ambayo hukuyafanya. Ni nadra kujutia jambo tulilofanya ambalo halikufanikiwa au tuliloshindwa," alisema.
8. Eleza mawazo yako
Mwandishi Brad Stone anaamini kwamba Mkurugenzi Mtendaji wa Amazon haamini katika demokrasia inapofika wakati wa kufanya maamuzi ya mwisho katika mikutano ya viongozi wa kampuni. Hata hivyo, Bezos pia anaamini kwamba ni muhimu kuwepo kwa mjadala wa wazi na wa ukweli.
John Rosman anaamini Amazon ni tofauti na kampuni nyingine zinazofanana nayo katika suala hili.
9. Shiriki katika ushindani
Bezos amekabiliana na ushindani mkubwa kutoka kwa kampuni nyingine za teknolojia. Brad Stone alitolea mfano wa teknolojia ya Alexa.
Apple ilipounda Siri, Google pia ilikuwa na uwezo wa kuunda msaidizi wa sauti wenye uwezo wa kueleza na kufanya mambo mbalimbali.
Alisema: "Amazon ilikuwa tayari kampuni kubwa na kiongozi katika teknolojia, lakini Jeff Bezos alisimamia mradi wa Alexa, ambao uliunda ajira 10,000 kwa sababu hakutaka kukata tamaa na kuruhusu kampuni nyingine zifanikiwe wakati huo."
10. Panga kwa ajili ya siku zijazo
Kupanga kwa muda mrefu kumekuwa sehemu muhimu ya mafanikio ya Bezos na Amazon.
John Rosman alisema Bezos "yuko tayari na ana subira ya kusubiri miaka 10 ili kupata faida, na amejitolea kufanikisha maendeleo anayoyaona mbele yake."