Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Iran yaweka masharti kabla ya kufungua tena Mlango Bahari wa Hormuz

Marekani, kwa upande wake, inaendelea kusisitiza kuwa Mlango wa Hormuz uko wazi na kwamba mabomu ya baharini yameondolewa, huku ikisema hakuna mazungumzo yaliyopangwa kwa sasa na Iran.

Moja kwa moja

Na Mariam Mjahid

  1. Trump aagiza Ziwa Ontario kuitwa Ziwa Amerika

    Rais wa Marekani Donald Trump ametia saini agizo la kiutendaji linalolenga kubadili jina la Ziwa Ontario na kuliita Ziwa Amerika.

    Hatua hiyo inakuja baada ya mazungumzo ya kibiashara kati ya Marekani na Canada kuvunjika wiki iliyopita, huku Marekani ikiweka ushuru wa asilimia 50 kwa bidhaa za Canada zenye thamani ya dola bilioni 20.

    Trump amekuwa akitishia mara kadhaa kubadili jina la ziwa hilo, ambalo ni miongoni mwa maziwa makuu matano yanayopatikana katika eneo la Marekani na Canada.

    Kwa mujibu wa agizo hilo, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Marekani imepewa siku 30 kusasisha jina hilo katika hifadhidata rasmi ya majina ya maeneo ya kijiografia nchini humo.

    Hata hivyo, Waziri Mkuu wa Canada, Mark Carney, amepinga hatua hiyo, akisema jina Ziwa Ontario lina historia ya zaidi ya miaka 400.

    Carney amesema ziwa hilo linaitwa Ontario na litaendelea kuitwa hivyo.

    Hii si mara ya kwanza kwa Trump kujaribu kubadili jina la eneo linaloshirikisha nchi nyingine. Mwaka 2025, alisaini agizo la kubadili jina la Ghuba ya Mexico kuwa Ghuba ya America, hatua ambayo Mexico imeikataa.

    Pia unaweza kusoma:

  2. Vyombo vya habari Marekani: Mkuu wa CIA aishinikiza Urusi kutoshirikisha Iran taarifa za kijasusi

    Vyanzo vilivyo na ufahamu kuhusu suala hilo vimeviambia vyombo vya habari vya Marekani kwamba Mkurugenzi wa Shirika la Ujasusi la Marekani, CIA, John Ratcliffe, aliiomba idara za ujasusi za Urusi kutoshirikisha Tehran taarifa ambazo zinaweza kuisaidia Iran, wakati wa ziara yake ya siri mjini Moscow.

    Inadaiwa pia kuwa suala la msaada wa Urusi kwa Iran lilikuwa miongoni mwa mada kuu zilizojadiliwa katika mazungumzo yake na maafisa wa Urusi.

    Ziara hiyo ni ya kwanza kwa mkuu wa CIA kwenda Moscow ambayo imefahamika hadharani tangu mwaka 2021. Kremlin imethibitisha kuwa Ratcliffe alikutana na maafisa wa ujasusi wa Urusi, lakini si Rais Vladimir Putin.

    Mbali na suala la Iran, Ratcliffe anaripotiwa kujadili pia wasiwasi wa Marekani kuhusu usalama wa wanachama wa NATO katika mazungumzo hayo.

    Hata hivyo, Marekani na Urusi hazijatoa maelezo rasmi kuhusu yaliyomo katika mazungumzo hayo, huku CIA ikikataa kutoa maoni kuhusu ziara hiyo.

    Rais wa Marekani, Donald Trump, aliielezea ziara hiyo kuwa ya "kawaida kwa kiasi" na kusema mawasiliano hayo yanaweza kusaidia kusukuma mbele baadhi ya masuala, likiwemo suala la kumaliza vita nchini Ukraine. Hakutoa maelezo zaidi kuhusu mazungumzo hayo.

    Ripoti kuhusu msaada wa kijasusi kutoka China na Urusi kwa Iran wakati wa vita kati ya Marekani, Israel na Iran zimeibuliwa mara kadhaa katika miezi ya hivi karibuni.

    Moscow nayo imekuwa ikiishutumu Marekani na washirika wake wa Ulaya kwa kuipatia Ukraine taarifa za kijasusi na imekuwa ikiitaka Washington kusitisha msaada huo.

    Maelezo zaidi:

  3. Idadi ya watu waliofariki Nepal na Tibet yafikia 469 huku kukiwa na hofu ya mafuriko zaidi

    Takriban watu 469 wamefariki dunia nchini Nepal na mamia hawajulikani walipo baada ya mafuriko makubwa ya ghafla yaliyokumba eneo la milimani mpakani mwa Nepal na Tibet Jumatano.

    Nchini Tibet, watu watatu wamefariki na zaidi ya 550 hawajulikani walipo. Haijafahamika iwapo baadhi ya watu hao wamehesabiwa pia katika takwimu za Nepal.

    Waokoaji wanaendelea kuwasaka manusura, lakini wanakabiliwa na hofu ya kutokea kwa mafuriko mengine katika eneo lililoharibiwa.

    Shirika la Msalaba Mwekundu limeiambia BBC kuwa waokoaji wako katika hali ya tahadhari kutokana na ripoti kwamba wimbi jingine la mafuriko linaweza kulikumba eneo hilo.

    Ziwa lenye maji yanayoongezeka limejitokeza karibu na mpaka wa China na Nepal, hali inayozua hofu kwamba huenda kingo zake zikapasuka na kusababisha mafuriko mengine.

    Maafisa wa eneo hilo wameiambia BBC kuwa kuporomoka kwa barafu ya mlima kulisababisha wimbi kubwa la maji lililosomba nyumba na barabara, pamoja na kuharibu kituo muhimu cha mpakani kinachounganisha Nepal na Tibet.

    Eneo hilo hutembelewa na makumi ya maelfu ya watalii kila mwaka.

    BBC imezungumza na ndugu za baadhi ya watu ambao bado hawajulikani walipo.

    Dada wawili ambao wazazi wao hawajulikani walipo wameeleza matumaini yao ya kuwaona tena, wakisema: "Tunawapenda sana na tunataka warudi nyumbani."

    Soma Zaidi hapa:

  4. Iran yaweka masharti kabla ya kufungua tena Mlango Bahari wa Hormuz

    Mkuu wa usalama wa Iran, Mohsen Rezaei, amesema Tehran inaandaa orodha ya masharti ambayo Marekani inapaswa kutimiza kabla ya Iran kuruhusu tena usafirishaji kupitia Mlango wa Bahari wa Hormuz.

    Amesema hatua hiyo imekuja kufuatia maombi kutoka kwa wapatanishi wanaojaribu kupunguza mvutano kati ya Iran na Marekani.

    Katika mazungumzo yake na Waziri Mkuu wa Qatar, Sheikh Mohammed bin Abdulrahman Al Thani, Spika wa Bunge la Iran, Mohammad Bagher Ghalibaf, amesema utawala wa Rais Donald Trump unafanya maamuzi yasiyo sahihi kwa kutegemea taarifa potofu.

    Ghalibaf amesema Washington lazima itekeleze ahadi zake chini ya MOU kabla ya hatua zaidi kuchukuliwa.

    Waziri Mkuu wa Qatar yuko Tehran katika juhudi za upatanishi, huku akijadili pamoja na viongozi wa Iran masuala muhimu, likiwemo suala la Mlango wa Hormuz na uwezekano wa kuanza tena kwa mazungumzo kati ya Tehran na Washington.

    Marekani, hata hivyo, inaendelea kusisitiza kuwa Mlango wa Hormuz uko wazi na kwamba mabomu ya baharini yameondolewa, huku ikisema hakuna mazungumzo yaliyopangwa kwa sasa na Iran.

    Soma Zaidi Hapa:

  5. Hujambo, natumai umzima na karibu kwa matangazo yetu ya moja kwa moja ya leo Ijumaa.