Kocha wa Liverpool afutwa kazi
Kocha wa Liverpool Arne Slot amefutwa kazi baada ya kuwa naye kwa misimu miwili.
Mholanzi Arne Slot, mwenye umri wa miaka 47, aliwaongoza Reds kutwaa taji lao la 20 la ligi katika msimu wake wa kwanza lakini wamejitahidi katika mwaka wake wa pili, wakimaliza katika nafasi ya tano kwenye Ligi Kuu.
Kocha wa Bournemouth aliyeondoka hivi karibuni, Andoni Iraola, ndiye anayeongoza kati ya wanaopigiwa upatu kuchukua nafasi ya Slot.
"Huu ulikuwa uamuzi mgumu kwetu kama klabu. Mchango wa Arne ndani ya Liverpool FC katika kipindi ambacho amekuwa nasi umekuwa muhimu, wenye maana na – cha msingi zaidi kwa mashabiki na sisi wenyewe - wenye mafanikio," wamiliki wa Liverpool Fenway Sports Group (FSG) walisema katika taarifa.
"Kwa hivyo, shukrani zetu kwa kila kitu alichofanikisha, haswa katika maadili ya kazi, bidii na kiwango cha utaalamu ambacho kilisisitiza zaidi mtazamo wetu kwamba yeye ni kiongozi katika tasnia yake."
"Tangu tulipokutana na Arne kwa mara ya kwanza, ilikuwa wazi mara moja kwamba yeye ni mtu ambaye hakubali tu jukumu, bali analikumbatia."
Uamuzi huo ulifanywa na Michael Edwards, mtendaji mkuu wa FSG, na Richard Hughes, mkurugenzi wa michezo wa Liverpool.
Katika msimu mzima, Liverpool ilisisitiza kwamba mabadiliko ya kocha mkuu hayakuwa kwenye ajenda, lakini baada ya kutathmini hali baada ya mwisho wa msimu wikendi iliyopita, uongozi wa klabu hiyo unaamini awamu inayofuata inahitaji mtindo wa soka ulioimara zaidi, wa kisasa na kwa haraka.
Slot alichukua nafasi ya Jurgen Klopp kama kocha wa Liverpool mwaka wa 2024 baada ya Mjerumani huyo kujiuzulu Anfield baada ya miaka tisa kama meneja.
Mapema mwezi huu, mshambuliaji Mohamed Salah alisema klabu hiyo lazima irudi kuwa "timu ya ushambuliaji wa kiwango cha juu ambayo wapinzani wanaiogopa" baada ya "kushindwa" na Aston Villa.
Pia unaweza kusoma: