Islamabad kuongoza mazungumzo ya Marekani na Iran leo, Iran bado haijathibitisha

Chanzo cha picha, Getty Images
Mazungumzo kati ya Marekani na Iran yanatarajiwa kuanza leo katika mji mkuu wa Pakistan, Islamabad.
Wageni katika Hoteli ya Serena ya mjini humo, ambako mazungumzo ya awali yaliyoshindwa kufikia makubaliano yalifanyika tarehe 11 Aprili, wameombwa kuondoka ili kuandaa mkutano wa leo. Polisi pia wametangaza kufungwa kwa barabara muhimu kutokana na ujio wa wajumbe hao wa mkutano.
Rais Donald Trump amesema “wajumbe wake” watawasili Islamabad Jumatatu jioni, akieleza kuwa Makamu wa Rais JD Vance ataongoza ujumbe huo pamoja na Steve Witkoff na Jared Kushner.
Hata hivyo, Iran bado haijathibitisha rasmi kama itashiriki katika mazungumzo hayo. Vyombo vya habari vya serikali ya Iran vinaripoti kuwa maafisa wake hawatashiriki mazungumzo iwapo vizuizi vya Marekani dhidi ya bandari za Iran vitaendelea.
Makubaliano ya kusitisha mapigano ya muda wa wiki mbili kati ya Marekani na Iran yanatarajiwa kumalizika Jumatano, huku Trump akiendelea kutoa vitisho vya kuharibu miundombinu ya Iran iwapo makubaliano hayatafikiwa.

Chanzo cha picha, Getty Images







