Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Nini hutokea ini lenye mafuta linaposhindwa kufanya kazi?
Kutokana na matatizo mbalimbali ya kiafya, ikiwemo usingizi kupita kiasi na kisukari, nilikwenda katika hospitali kubwa binafsi mjini Colombo kwa ajili ya uchunguzi.
Huko, baada ya kufanyiwa vipimo kadhaa na iligundulika kuwa nilikuwa na ugonjwa wa ini lenye mafuta (fatty liver disease) katika hatua ya pili.
"Acha kunywa pombe mara moja," daktari mmoja aliyekuwa akinifanyia vipimo alinshauri.
Hata hivyo, mimi si mnywaji wa pombe. Lakini pamoja na hilo, ini langu lilikuwa limeathirika.
Ini ni kiungo muhimu sana katika mwili wa binadamu, na ni muhimu kuelewa kazi zake kwa sababu linapopatwa na ugonjwa au kushindwa kufanya kazi ipasavyo, linaweza kusababisha matatizo mbalimbali ya afya.
Ini lenye mafuta ni nini? Na, husababishwa na nini?
"Kujikusanya kwa mafuta ndani ya ini ugonjwa unaoitwa ini lenye mafuta (Fatty Liver). Ugonjwa huu unaweza kutokea kwa watu wanaokunywa pombe na pia kwa wasiokunywa pombe.
Kulingana na Chuo cha Tiba ya Magonjwa ya Ndani cha Sri Lanka hali hizi zinajulikana kama Alcoholic Fatty Liver na Non-Alcoholic Fatty Liver mtawalia.
Kwa hiyo, ni wazi kwamba ugonjwa wa ini lenye mafuta unaweza kusababishwa pia na sababu nyingine mbali na matumizi ya pombe.
Matumizi ya pombe huathiri moja kwa moja hali ya ini lenye mafuta linalohusishwa na pombe (Alcoholic Fatty Liver Disease).
Hata hivyo, kuna sababu nyingi zinazochangia hali inayojulikana kama ugonjwa wa ini lenye mafuta unaohusishwa na matatizo ya kimetaboli (Metabolic Dysfunction-Associated Steatotic Liver Disease - MASLD).
Mambo yanayoathiri ini lenye mafuta kwa asiyekunywa pombe
Chuo cha Madaktari wa Tiba ya Ndani cha Sri Lanka kinasema kuwa magonjwa mbalimbali, mifumo ya ulaji, hali za mwili, na sababu nyingine zinaweza kuathiri hali ya kwa mtu asiyekunywa pombe.
Baadhi ya sababu hizo ni:
- Kisukari
- Kutofanya mazoezi
- Ulaji kupita kiasi wa vyakula vilivyosindikwa vyenye fructose na mafuta mengi
- Kurithi kutoka kwa wazazi kwenda kwa watoto kupitia vinasaba (jeni)
- Unene kupita kiasi
Ikiwa una mojawapo ya sababu zilizotajwa hapo juu, una hatari kubwa zaidi ya kupata ugonjwa wa ini lenye mafuta. Ingawa ugonjwa huu hupatikana zaidi kwa watu wenye unene kupita kiasi, Chuo cha Madaktari wa Tiba ya Ndani cha Sri Lanka kinaeleza kuwa hata watu wenye uzito mdogo au waliokonda wanaweza kuupata ugonjwa huu.
Ni vipimo gani vinavyoweza kutumika kuchunguza uwepo wa mafuta kwenye ini?
Kuna vipimo kadhaa vinavyoweza kutumika kuchunguza ugonjwa wa ini lenye mafuta mengi.
Profesa Arjuna de Silva anasema kuwa uchunguzi wa awali unaweza kufanywa kupitia Kipimo cha Utendaji Kazi wa Ini (LFT), ambacho hufanyika ili kuangalia jinsi ini linavyofanya kazi.
Aidha, hali hiyo inaweza pia kugunduliwa kwa kutumia kipimo cha 'ultrasound'.
Profesa huyo pia alibainisha kuwa uwezekano wa ugonjwa wa ini lenye mafuta kuendelea na kuwa 'cirrhosis' (ugonjwa sugu wa ini ambapo tishu za kawaida hubadilika na kuwa tishu ngumu za kovu) unaweza kugunduliwa kupitia kipimo cha "FibroScan".
Alisema kuwa kipimo hicho kinaweza kubaini kiasi cha mafuta yaliyopo kwenye ini pamoja na uharibifu wowote wa ini.
Je, maradhi ya ini lenye mafuta hupitia hatua zipi?
Ukuaji wa ugonjwa wa ini lenye mafuta hugawanywa katika hatua nne.
Hali ya kawaida ya ini kuwa na mafuta (Steatosis) - hatua ya awali ya mkusanyiko wa mafuta kwenye ini
Steatohepatitis - hatua ya awali ya uharibifu wa seli za ini
Fibrosis - hatua ya kutokea kwa tishu ngumu za kovu kuzunguka ini na mishipa ya damu
Cirrhosis - hatua ya kusinyaa kwa ini na kushindwa kufanya kazi vizuri
Profesa Arjuna de Silva anasema kuwa inaweza kuchukua takriban miaka 20 kwa ugonjwa huo kuendelea kutoka hatua ya kawaida ya ini kuwa na mafuta hadi kufikia hatua ya 'cirrhosis'.
Hata hivyo, muda huo hutegemea kiasi cha mambo hatari yanayochangia hali hiyo, ikiwa ni pamoja na matumizi ya pombe.
Ni nini hutokea iwapo ini litashindwa kufanya kazi?
Nilipokuwa mtoto, nilifahamu kuwa ndugu yangu mmoja alikuwa na tumbo lililovimba kwa namna isiyo ya kawaida, na alikuwa na ugonjwa wa 'cirrhosis'.
Kwa ninavyoelewa, alikuwa na 'cirrhosis' iliyosababishwa na matumizi ya pombe.
Niliona kuwa ingawa alipata nafuu kiasi baada ya kupata matibabu kwa muda mrefu, usaha ulianza kutoka tumboni mwake baada ya muda mfupi.
Sababu ya hali hiyo, kama nilivyoelezwa na wazee, ni kwamba hali kama hiyo inaweza kutokea kwa sababu ini linashindwa kufanya kazi na viungo vingi vya mwili hupoteza uwezo wa kufanya kazi ipasavyo.
Profesa Arjuna de Silva alielezea athari za kushindwa kufanya kazi kwa ini mwilini mwetu kama ifuatavyo.
"Ini linawajibika kwa michakato mingi ya mwili. Karibu kila kitu mwilini huzalishwa kwenye ini. Ini hudhibiti mafuta mwilini. Ini ni muhimu kwa udhibiti wa glukosi. Ikiwa sumu imemezwa, ini huitoa makali yake. Pombe ni sumu. Ini huharibika mara tu inapoharibiwa. Kwa hivyo ikiwa ini litaathirika, matatizo mengi yanaweza kutokea.
Kwa hivyo, kushindwa kwa ini kunaweza kusababisha matatizo kadhaa ya kiafya, ikiwa ni pamoja na cirrhosis, saratani ya ini, na magonjwa ya moyo na mishipa kama vile ugonjwa wa moyo.
Je, tatizo la ini lenye mafuta linaweza kutibika?
Profesa Arjuna de Silva anasema kuwa hata katika hatua ya tatu ya ugonjwa wa ugumu wa tishu za ini), ini linaweza kurejea katika hali ya afya ya asilimia 100 likipatiwa matibabu sahihi.
Aidha, alibainisha kuwa tofauti na viungo vingine, ini lina uwezo wa kujijenga upya likitibiwa ipasavyo.
"Kuna jambo la kipekee. Ukiondoa kiungo kingine kama figo, hakiwezi kuota tena. Hata sehemu ya figo haiwezi kupandikizwa; ni lazima kupandikiza figo nzima. Lakini unapopandikiza ini, si lazima kufanya hivyo."
Jinsi ya kuzuia tatizo la ini lenye mafuta?
Tatizo hili linaweza kuzuiwa kwa kufuata mtindo sahihi wa maisha, kula mlo kamili na wenye afya, na kushiriki katika shughuli mbalimbali, ikiwemo mazoezi. Hasa:
Acha kunywa pombe.
Dhibiti magonjwa kama kisukari na kiwango cha kolesteroli.
Dumisha uzito sahihi wa mwili (kulingana na kipimo cha BMI).
Fanya mazoezi.
Fuata lishe bora.
Fanya vipimo vya ini na utafute matibabu ikihitajika.