Tume ya vurugu za uchaguzi Tanzania yapokea ushahidi
Mwenyekiti wa Tume ya Uchunguzi wa Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, Jaji Chande, amesema tume hiyo imepokea ushahidi kutoka kwa Watanzania 63,603 kupitia njia mbalimbali.
Amesema ushahidi huo umetolewa kupitia mahojiano ya ana kwa ana ya watu 1,323, mashahidi wa viapo (affidavits) 553, madodoso yasiyo na majina ya watu 4,891, mikutano na makundi 202, pamoja na simu na ujumbe mfupi kutoka kwa watu 56,445.
Kulingana na Jaji Chande, wote hao wametoa taarifa kuhusu matukio ya uvunjifu wa amani yaliyotokea katika kipindi hicho.
Kumekuwa na madai kutoka kwa baadhi ya wadau hasa wanaharakati mitandaoni nchini Tanzania wanaoona kwamba kuongezwa kwa muda wa tume hiyo mara mbili kunalenga kutoa nafasi kwa mamlaka fulani 'kuchakachua' yaliyomo kwenye ripoti hiyo.
Hata hivyo, Jaji Chande alieleza kuwa sababu kuu ya kuongeza muda ni kupanuka kwa wigo wa kazi pamoja na ongezeko la ushahidi unaokusanywa.
Ripoti kamili ya uchunguzi huo inatarajiwa kuwasilishwa tarehe 23 Aprili 2026.