Mamlaka nchini Zambia zimemkamata raia wa Kenya mwenye umri wa miaka 56, Michael Njuka, anayefahamika pia kama Michael Juga, kwa tuhuma za kuhusika katika njama ya kutekeleza mashambulizi ya kimtandao dhidi ya serikali na kulenga miundombinu ya uchaguzi nchini humo.
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu katika Wizara ya Mambo ya Ndani na Usalama wa Ndani ya Zambia, Dickson Matembo, Njuka alikamatwa Jumatano katika operesheni ya pamoja iliyofanywa na vyombo vya ulinzi na usalama, siku chache kabla ya uchaguzi mkuu wa Zambia wa Agosti 13, 2026.
Akizungumza kuhusu kukamatwa kwa Njuka, Matembo alisema: “Katika tukio linalohusiana na hili, serikali imemkamata raia wa Kenya aliyetambuliwa kama Michael Njuka, mwenye umri wa miaka 56, ambaye anadaiwa kuwa amepewa kandarasi ya kutekeleza uhalifu wa kimtandao unaolenga serikali.”
Kwa mujibu wa chombo cha habari cha Kenya NTV, mamlaka zinasema Njuka na washukiwa wengine wawili walikuwa wamepewa kandarasi ya kutekeleza uhalifu wa kimtandao dhidi ya serikali, kwa lengo la kuhujumu miundombinu ya uchaguzi.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, Matembo alisema, “Baada ya operesheni iliyofanikiwa, serikali imewakamata maafisa watatu wa zamani wa ngazi za juu serikalini kwa madai ya kutoa huduma za kiufundi zilizolenga kuvuruga mfumo wa uchaguzi. Watatu hao kwa sasa wanashikiliwa chini ya ulinzi halali wa serikali.”
Maafisa hao ni Japhern Mwakalombe, Mwila Kakana na Sensho Banda, ambao wizara imesema wanasaidia katika uchunguzi unaoendelea.
Kwa mujibu wa mamlaka, washukiwa hao walikutwa wakiwa na dola za Marekani 387,500.
Hata hivyo, mamlaka hazijaeleza chanzo cha fedha hizo wala madhumuni yaliyokusudiwa.
Matembo pia alisema uchunguzi umebaini kuwepo kwa taarifa nyeti za kijeshi katika baadhi ya vifaa vya kielektroniki vilivyokamatwa kutoka kwa washukiwa, hali iliyozua wasiwasi kuhusu uwezekano wa watu wasioidhinishwa kupata taarifa zinazolindwa.
Kuhusu kukamatwa kwa Njuka, Matembo alisema raia huyo wa Kenya anadaiwa kupewa kandarasi ya kutekeleza uhalifu wa kimtandao uliolenga serikali.
Mamlaka za ulinzi na usalama nchini Zambia zimesema zimeongeza tahadhari ili kulinda mchakato wa uchaguzi na usalama wa taifa dhidi ya hujuma za kimtandao au za kimwili.
Rais wa Zambia na kiongozi wa chama tawala cha United Party for National Development, Hakainde Hichilema, alikuwa akiwania muhula mwingine akisisitiza ajenda ya kufufua uchumi, kuboresha huduma za umma na kuongeza ajira kwa vijana.
Hichilema anashindana na wagombea wengine 13 katika uchaguzi huo, uliokuwa muhimu kwa Zambia inayojulikana kwa historia ya chaguzi zinazochukuliwa kuwa za amani na za kuaminika.