Marekani imemfungulia mashtaka kiongozi wa zamani wa Cuba Raul Castro

Chanzo cha picha, Reuters
Marekani imemshtaki kiongozi wa zamani wa Cuba, Raul Castro, kwa kupanga kuwaua raia wa Marekani na makosa mengine yaliyotokana na kuangushwa kwa ndege mbili zilizokuwa zikifanya safari kutoka eneo la Florida hadi Cuba.
Kesi hiyo inamshtumu Castro na watu wengine watano kwa kuhusika kuzifyatulia risasi ndege hizo, zilizokuwa zinamilikiwa na kundi la Cuba-America Group Brothers, na kuwauwa watu wanne, watatu wakiwa raia wa Marekani.
Castro, kwa sasa ana umri wa miaka 94, na wakati huo alikuwa mkuu wa majeshi ya Cuba na alikashifiwa vikali kimataifa baada ya tukio hilo.
Wakati Marekani inaendelea kuongeza shinikizo dhidi ya utawala wa kikomunisti wa Cuba, Rais Miguel Díaz-Canel ameelezea mashtaka hayo kama “shinikizo la kisiasa, usio na msingi wa kisheria.”
Akizungumza katika jengo la Freedom Tower mjini Miami, Mwanasheria Mkuu wa Marekani Todd Blanche, alitangaza kuwa taifa lake litamfungulia Castro mashtaka ya uharibifu wa ndege na makosa manne ya mauaji .
“Marekani, na Rais Trump, haisahau wala haitasahau raia wake,” Blanche alisema.
Mashtaka hayo yatasikizwa katika mahakama za Marekani, na kila shtaka la mauaji linaweza kuwa na adhabu ya kifo au kifungo cha maisha.
Pia unaweza kusoma:



