Kundi la kwanza la wahamiaji lawasili DRC kutoka Marekani chini ya makubaliano mapya
Kundi la kwanza la wahamiaji waliorejeshwa kutoka Marekani chini ya makubaliano mapya ya pande mbili limewasili mapema Ijumaa nchini Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC), reuters inaripoti.
Ndege iliyobeba wahamiaji kutoka Colombia, Peru na Ecuador ilitua mjini Kinshasa majira ya saa 1:00 usiku. Mwanamke mmoja kutoka Colombia alisema kulikuwa na wahamiaji 16, wanaume tisa na wanawake saba, ingawa chanzo kimoja kutoka uwanja wa ndege kilitaja idadi ya wahamiaji 15. Mamlaka za serikali ya Congo hazikutoa tamko mara moja kuhusu tukio hilo.
Ripoti zilieleza kuwa zaidi ya wahamiaji 30 walitarajiwa kuwasili DRC wiki hii, lakini wakili mmoja wa Marekani alisema idadi hiyo ndogo huenda imesababishwa na maamuzi ya dakika za mwisho ya majaji wanaoshughulikia uhamisho huo.
Mmoja wa wahamiaji alisema safari hiyo ilikuwa ndefu sana, ikichukua takribani saa 26 hadi 27, lakini walihudumiwa vizuri ndani ya ndege. Taarifa za safari zinaonyesha ndege ilianzia Alexandria, Louisiana, na kupita Dakar, Senegal pamoja na Accra, Ghana kabla ya kufika Kinshasa.
Huu ni uhamisho wa kwanza wa wahamiaji wa nchi nchingine kupelekwa DRC, taifa linalokabiliwa na changamoto za usalama, wakimbizi wa ndani na mfumo dhaifu wa hifadhi ya wakimbizi. Makubaliano hayo pia yanakwenda sambamba na juhudi za Marekani kusukuma makubaliano ya amani kati ya DRC na Rwanda ili kumaliza mapigano mashariki mwa nchi.