Shambulio kubwa la Urusi dhidi ya Ukraine laua watu wanne na kujeruhi makumi
Urusi imefanya mashambulizi makubwa na ya maangamizi dhidi ya Ukraine usiku wa kuamkia Jumamosi, ikirusha mamia ya droni na makombora kadhaa.
Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelenskyy, amesema mji mkuu Kyiv ndio ulikuwa shabaha kuu, ingawa maeneo mengine pia yalilengwa, huku takribani watu 100 wakijeruhiwa.
Watu wanne waliuawa katika mji mkuu na maeneo ya karibu, huku milipuko ikisikika usiku kucha.
Mamia ya majengo ya makazi, shule, nyumba ya opera na jumba la makumbusho yaliharibiwa.
Wizara ya Ulinzi ya Urusi imesema kuwa ilitumia kombora la hypersonic aina ya Oreshnik katika mashambulizi hayo, ambayo ilieleza kuwa ni kujibu “mashambulizi ya Ukraine dhidi ya miundombinu ya kiraia”. Hata hivyo, jeshi la Ukraine limekanusha kulenga raia.
Mapema Jumatatu, miundombinu ya nishati iliharibiwa katika shambulio la makombora katika eneo la Belgorod nchini Urusi linalopakana na Ukraine, ikiwa ni pamoja na mji wa Belgorod, kwa mujibu wa shirika la habari la Interfax likinukuu mamlaka za eneo hilo.
Hakukuwa na vifo vilivyoripotiwa, lakini huduma za umeme na maji zilikatika, taarifa hiyo ilisema.
Eneo la Yaroslavl nchini Urusi, kaskazini mashariki mwa Moscow, pia lililengwa na mashambulizi ya droni, gavana wake Mikhail Yevrayev alisema kupitia Telegram.
Rais wa Urusi Vladimir Putin alianzisha uvamizi mkubwa dhidi ya Ukraine Februari 2022.
Jeshi la Ukraine limesema pia lilifanya shambulio katika eneo la Starobilsk lililoko mashariki mwa Ukraine linalodhibitiwa na Urusi usiku wa Ijumaa, likieleza kuwa lililenga kitengo maalum cha kijeshi cha droni cha Urusi.
Viongozi wa Ulaya wamelaani mashambulizi hayo ya Urusi yaliyofanyika mapema Jumapili, yakija baada ya onyo la Zelensky kwamba Urusi ilikuwa inapanga mashambulizi mapya na huenda ilijiandaa kutumia kombora la Oreshnik.
Inaripotiwa kuwa kombora hilo husafiri kwa kasi zaidi ya mara 10 ya sauti, ni vigumu kulizuia, na lina uwezo wa kubeba vichwa vya kawaida na vya nyuklia.
Soma zaidi: