Mwanaanga wa China kuishi mwaka mzima anga za juu huku Beijing ikijipanga kuelekea Mwezini

Chanzo cha picha, CMSA/CCTV)
China imezindua safari mpya ya anga za juu inayojumuisha watu watatu kuelekea kituo chake cha anga cha Tiangong Space Station, ambapo mmoja wa wanaanga hao atatumia mwaka mzima akiwa katika mzunguko wa Dunia.
Hatua hiyo inachukuliwa kuwa sehemu muhimu ya maandalizi ya mpango wa Beijing wa kupeleka binadamu Mwezini ifikapo mwaka 2030.
Misheni hiyo, inayojulikana kama Shenzhou-23, imezinduliwa siku ya Jumapili kwa kutumia roketi ya Long March 2F kutoka kituo cha kurushia vyombo vya anga cha Jiuquan kilichopo katika Jangwa la Gobi, kaskazini magharibi mwa China.
Katika kipindi cha miongo mitatu iliyopita, China imewekeza mabilioni ya dola katika sekta ya anga huku ikilenga kujiimarisha kama moja ya mataifa yanayoongoza katika uchunguzi wa anga za juu.
Tangu mwaka 2021, misheni za Shenzhou zimekuwa zikituma wanaanga watatu kwa wakati mmoja katika kituo cha Tiangong kwa safari za takribani miezi sita. Hata hivyo, safari hii itakuwa ya kipekee kwa kuwa itashuhudia mwanaanga mmoja akibaki angani kwa muda wa mwaka mzima kwa mara ya kwanza katika historia ya mpango wa anga wa China.
Miongoni mwa wanaanga walioko katika misheni hiyo ni Li Jiaying mwenye umri wa miaka 43, ambaye amekuwa mwanaanga wa kwanza kutoka Hong Kong kushiriki katika safari ya anga. Kabla ya kujiunga na mpango wa anga wa China, Li aliwahi kufanya kazi katika jeshi la polisi la Hong Kong.
Wanachama wengine wa misheni hio ni Zhu Yangzhu, mhandisi wa anga mwenye umri wa miaka 39, na Zhang Zhiyuan, mwenye umri wa miaka 39 na aliyekuwa rubani wa Jeshi la Anga la China. Kwa wote wawili, hii ni safari yao ya kwanza kwenda angani.
Wakiwa katika kituo cha Tiangong, wanaanga hao wanatarajiwa kutekeleza miradi mbalimbali ya kisayansi inayohusu sayansi ya maisha, sayansi ya vifaa, fizikia ya vimiminika na tiba.
Jaribio muhimu zaidi katika misheni ya Shenzhou 23 ni kufuatilia athari za kukaa kwa muda mrefu katika mazingira yenye mvutano mdogo wa nguvu za uvutano yaani gravity. Utafiti huo unalenga kusaidia maandalizi ya safari za baadaye za kuelekea Mwezini na hata sayari ya Mirihi.
Shirika la Anga la China limesema kuwa mwanaanga atakayechaguliwa kubaki angani kwa mwaka mmoja atatangazwa baadaye kulingana na maendeleo ya misheni hiyo.
Mtaalamu wa unajimu na profesa katika Chuo Kikuu cha Macquarie nchini Australia, Richard de Grijs, amesema changamoto kuu za safari za muda mrefu angani ni pamoja na kupungua kwa msongamano wa mifupa, kudhoofika kwa misuli, kuathiriwa na mionzi ya anga, matatizo ya usingizi pamoja na uchovu wa kisaikolojia na kitabia.
Ameongeza kuwa mifumo ya uhakika ya kuchakata maji na hewa, pamoja na uwezo wa kukabiliana na dharura za kiafya mbali na Dunia, ni mambo muhimu yatakayochangia mafanikio ya safari za muda mrefu za anga katika siku zijazo.
Soma zaidi:





