Moja kwa moja, Jeshi la Marekani lasema limefanya mashambulizi mapya kusini mwa Iran

Jeshi la Marekani limesema kuwa lililenga vituo vya kurushia makombora kusini mwa Iran pamoja na boti zilizokuwa zikijaribu kutega mabomu ya majini.

Moja kwa moja

Na Mariam Mjahid

  1. Marekani yasitisha mauzo ya silaha za dola bilioni 14 kwa Taiwan kutokana na vita vya Iran

    Hong Kao ameteuliwa kuwa kaimu katibu wa Jeshi la Wanamaji la Marekani tangu Aprili.

    Chanzo cha picha, CQ-Roll Call, Inc. via Getty Images

    Maelezo ya picha, Hong Kao ameteuliwa kuwa kaimu katibu wa Jeshi la Wanamaji la Marekani tangu Aprili.

    Marekani imesema imesitisha kwa muda mauzo ya silaha yenye thamani ya dola bilioni 14 kwa Taiwan ili kuhakikisha ina akiba ya kutosha ya silaha na risasi kwa ajili ya uwezekano wa vita dhidi ya Iran.

    Kaimu Katibu wa Jeshi la Wanamaji la Marekani, Hong Kao, amethibitisha hatua hiyo wakati wa kikao cha Kamati ya Seneti kilichofanyika jana.

    Hatua hiyo imekuja licha ya Rais wa Marekani, Donald Trump, kutotoa msimamo wa wazi kuhusu mauzo hayo siku chache zilizopita, akisema angejadili suala hilo na Rais wa Taiwan.

    Ofisi ya Rais wa Taiwan imesema Ijumaa kwamba haijapokea taarifa yoyote kuhusu kile ilichokiita “mabadiliko katika mchakato wa mauzo ya silaha wa Marekani”.

    Kwa muda mrefu, mauzo ya silaha za Marekani kwa Taiwan yamekuwa chanzo cha mvutano kati ya Washington na Beijing. China inaichukulia Taiwan kuwa sehemu ya eneo lake na haitambui utawala wake wa kujitegemea, huku ikiwa haijaondoa uwezekano wa kutumia nguvu kuirejesha chini ya udhibiti wake.

    “Tumesitisha mauzo haya kwa sasa ili kuhakikisha tuna risasi na vifaa vya kutosha kwa ajili ya Operesheni Epic Fury dhidi ya Iran, na bila shaka kuhakikisha tuna akiba ya kutosha,” Hong Kao aliiambia Seneti.

    Alipoulizwa kuhusu msimamo wa Taiwan kufuatia uamuzi huo wa Marekani, alisema bado hajazungumza na maafisa wa Taiwan.

    “Tunachofanya ni kuhakikisha tuna kila kitu tunachohitaji. Serikali itakapoona inafaa, mauzo ya silaha kwa mataifa ya kigeni yataendelea tena,” alisema.

    Soma zaidi:

  2. Netanyahu: Israel itaongeza mashambulizi dhidi ya Hezbollah

    g

    Chanzo cha picha, ge

    Jeshi la Israel limesema limeanzisha wimbi jipya la mashambulizi kote nchini Lebanon, baada ya Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, kutangaza kuwa nchi yake itaongeza mashambulizi dhidi ya kundi la Hezbollah.

    Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF) limesema limetekeleza mashambulizi dhidi ya malengo ya Hezbollah katika Bonde la Bekaa mashariki mwa Lebanon pamoja na maeneo mengine ya nchi hiyo.

    Kwa upande wake, Hezbollah imesema imejibu mashambulizi hayo kwa kutekeleza mashambulizi 22 kwa kutumia droni na makombora, ikidai kulenga wanajeshi wa Israel, vifaru, kambi za kijeshi na majengo mbalimbali.

    Mapema mwezi huu, Lebanon na Israel zilikubaliana kuongeza muda wa usitishaji mapigano kwa siku 45, ingawa mapigano katika baadhi ya maeneo yameendelea kuripotiwa.

    Katika ujumbe wa video alioutoa Jumatatu jioni, Netanyahu amesema Israel “iko vitani na Hezbollah” na kwamba jeshi limeagizwa “kulipiga kundi hilo pigo kubwa na la kuangamiza.”

    Alisema operesheni za kijeshi za Israel dhidi ya Hezbollah tayari “zimewaondoa zaidi ya magaidi 600,” lakini akasisitiza kuwa hatua inayofuata ni kuongeza kasi na ukubwa wa mashambulizi.

    “Lakini kile kinachohitajika sasa ni kuongeza mashambulizi na kuongeza nguvu ya operesheni hizi,” amesema Netanyahu.

    Waziri wa Fedha wa Israel, Bezalel Smotrich, na Waziri wa Usalama wa Taifa, Itamar Ben-Gvir, ambao wote wanatoka mrengo mkali wa kulia, wameitaka serikali kupanua operesheni za kijeshi, ikiwemo kuzifikisha hadi mji mkuu wa Lebanon, Beirut.

    Wakati huo huo, Israel imeendelea kutoa maonyo ya karibu kila siku kwa wakazi wa maeneo mapya kusini mwa Lebanon kuondoka makwao, hali iliyochangia kuongezeka kwa idadi ya watu waliokimbia makazi yao hadi zaidi ya milioni moja.

    Lebanon iliingia katika awamu hii ya mzozo baada ya Marekani na Israel kuanzisha vita dhidi ya Iran mnamo Februari 28. Hezbollah, mshirika wa karibu wa Iran, ilirusha makombora kuelekea Israel kujibu shambulio la Israel lililomuua Kiongozi Mkuu wa Iran, Ayatollah Ali Khamenei.

    Israel ilijibu kwa mashambulizi ya anga kote Lebanon na baadaye kuanzisha operesheni za ardhini. Kwa mujibu wa Wizara ya Afya ya Lebanon, zaidi ya watu 3,000 wameuawa katika mashambulizi ya Israel tangu kuanza kwa mapigano hayo.

    Serikali ya Lebanon imekuwa ikifanya juhudi za kulivua Hezbollah silaha, lakini imesema kuwa utekelezaji wa mpango huo unategemea kuwepo kwa usitishaji mapigano wa kudumu kutokana na ugumu wa mchakato huo.

    Soma zaidi:

  3. Rais wa Iran aagiza kurejeshwa kwa huduma za intaneti nchini humo

    f

    Chanzo cha picha, NurPhoto via Getty Images

    Rais wa Iran, Masoud Pezeshkian, ameagiza Wizara ya Mawasiliano kurejesha huduma za intaneti nchini katika hali iliyokuwapo kabla ya Desemba 2025.

    Naibu Waziri wa Mawasiliano amethibitisha kupokea agizo hilo, akisema kuwa hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za kurejesha haki za wananchi na kuimarisha imani ya umma kwa serikali.

    Vyombo vya habari vya serikali ya Iran vimeripoti kuwa katika kikao kilichoongozwa na Makamu wa Rais, Mohammad Reza Aref, maamuzi muhimu kuhusu hali ya intaneti nchini yaliidhinishwa.

    Taarifa hiyo ilieleza kuwa baada ya idhini ya mwisho kutoka kwa Rais Pezeshkian, maagizo rasmi yatatolewa kwa Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari ili kuyatekeleza.

    Kwa mujibu wa shirika la habari la Fars, pendekezo la kurejesha huduma za intaneti liliidhinishwa kwa kura tisa za kuunga mkono na baadaye kuwasilishwa katika ofisi ya rais kwa ajili ya idhini ya mwisho.

    Huduma za intaneti nchini Iran zilisitishwa wakati wa operesheni za kukabiliana na maandamano yaliyotokea Desemba mwaka jana.

    Baadaye, zilipunguzwa tena kufuatia mashambulizi yaliyotekelezwa na Israel na Marekani dhidi ya Iran. Hatua ya sasa inaashiria uwezekano wa kurejea kwa huduma za mawasiliano kwa kiwango kikubwa baada ya miezi kadhaa ya vikwazo.

    Pia unaweza kusoma:

  4. Trump: Urani iliyorutubishwa itakabidhiwa Marekani au kuharibiwa kwa ushirikiano na Iran

    g

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema kuwa urani iliyorutubishwa nchini Iran itakabidhiwa mara moja kwa Marekani ili isafirishwe na kuharibiwa, au itaharibiwa katika eneo jingine litakalokubaliwa kwa ushirikiano kati ya Marekani na Iran.

    Katika ujumbe aliouchapisha kwenye mtandao wake wa Truth Social, Trump amesema mchakato huo utafanyika chini ya uangalizi wa mamlaka husika za nishati ya atomiki au taasisi nyingine inayolingana na jukumu hilo.

    Katika ujumbe mwingine kwenye mtandao huo, Trump amechapisha michoro miwili inayolinganisha sera za Marekani dhidi ya Iran.

    Mchoro wa kwanza ulionyesha rundo la fedha ukiwa na maelezo: “Sera ya Iran ya Obama”, akimrejelea rais wa zamani wa Marekani, Barack Obama.

    Mchoro wa pili umeonyesha meli ya kivita ya Marekani ikishambuliwa kwa mabomu ukiwa na maelezo: “Sera ya Iran ya Trump.”

    Kauli za Trump zimekuja wakati jeshi la Marekani likiwa limetekeleza mashambulizi mapya kusini mwa Iran, hatua inayoongeza mvutano licha ya mazungumzo yanayoendelea kati ya Washington na Tehran.

    Pia unaweza kusoma:

  5. Jeshi la Marekani lasema limefanya mashambulizi mapya kusini mwa Iran

    f

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Jeshi la Marekani limesema limefanya mashambulizi mapya kusini mwa Iran, likilenga maeneo ya makombora ya Iran pamoja na boti zilizokuwa zikijaribu kuweka mabomu ya majini.

    Kamandi Kuu ya Jeshi la Marekani (CENTCOM) imesema katika taarifa kwamba mashambulizi hayo yalifanywa kwa lengo la kujilinda na yalikusudiwa “kulinda wanajeshi wetu dhidi ya vitisho vinavyotokana na vikosi vya Iran.”

    Msemaji wa CENTCOM, Kapteni Tim Hawkins, alisema jeshi la Marekani linaendelea kulinda vikosi vyake huku likionyesha kujizuia wakati wa kipindi cha usitishaji mapigano kinachoendelea.

    Mashambulizi hayo yamefanyika wakati msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmail Baghaei, akisema kuwa kuna maendeleo fulani yaliyopatikana katika mazungumzo na Marekani, lakini akasisitiza kuwa makubaliano ya kumaliza mzozo huo “hayako karibu kufikiwa.”

    Kwa mujibu wa Kapteni Hawkins, mashambulizi hayo yalilenga eneo karibu na Bandar Abbas, mji wa bandari ulioko kusini mwa Iran na makao ya kambi ya jeshi la wanamaji la Iran katika Mlango Bahari wa Hormuz.

    Vyombo vya habari vya serikali ya Iran vilikuwa vimeripoti awali kuwa maafisa wa eneo hilo walikuwa wakichunguza chanzo cha milipuko iliyosikika katika Bandar Abbas.

    Hadi sasa, Iran haijatoa tamko rasmi kuhusu mashambulizi hayo ya karibuni ya Marekani. Pia haijafahamika ni athari gani mashambulizi hayo yanaweza kuwa nayo kwa juhudi za kufikia makubaliano ya amani kati ya Washington na Tehran.

    Mwishoni mwa wiki, Rais wa Marekani, Donald Trump, alikuwa ameashiria kuwa pande hizo zilikuwa karibu kufikia makubaliano, lakini baadaye alisema amewaagiza wapatanishi wa Marekani kutoharakisha mchakato huo.

    Marekani na Iran zimekuwa zikiheshimu usitishaji mapigano tangu Aprili 8. Hata hivyo, Iran imeendelea kudhibiti usafiri wa majini katika Ghuba kupitia Mlango Bahari wa Hormuz, huku Jeshi la Wanamaji la Marekani likijaribu kuzuia shughuli za bandari za Iran.

    Mzozo huo ulianza Februari 28 baada ya Marekani na Israel kufanya mashambulizi makubwa dhidi ya Iran.

    Tehran ilijibu kwa kushambulia Israel na baadhi ya mataifa washirika wa Marekani katika Ghuba, pamoja na kuzuia kwa kiasi kikubwa usafiri wa majini katika Mlango Bahari wa Hormuz, hatua iliyochangia kupanda kwa bei ya mafuta duniani.

    Pia unaweza kusoma:

  6. Hujambo na karibu kwa matangazo ya moja kwa moja ya Jumanne tarehe 26 Mei 2026.