Ugunduzi wa bahati wa Viagra ambao ulibadilisha ulimwengu

Chanzo cha picha, Getty Images
Uvumbuzi wa Viagra ulikuwa wakati muhimu katika historia ya ngono, lakini cha kufurahisha, ilikuwa uvumbuzi wa bahati mbaya ambao ulitokea wakati wa jaribio ambalo lilikuwa na kitu kingine akilini.
Viagra ilianza kuuzwa mnamo 1998 na mara moja ikawa dawa iliyouzwa sana.
'Kidonge cha bluu' kilichogunduliwa kwa bahati mbaya na kampuni ya dawa ya Marekani ya Pfizer ikawa chanzo kikubwa ya kuwaingizia pesa.
Katika miezi mitatu ya kwanza pekee, Wamarekani walitumia wastani wa dola milioni 400 kununua dawa hiyo ya kuongeza nguvu za kiume.
Viagra: Hadithi ya ugunduzi ambao haukutarajiwa
Dkt. Mitra Bollil, anayefanya kazi katika idara ya utafiti ya Pfizer nchini Uingereza, aliiambia BBC Brazil kwamba dawa iliyotumiwa leo kuboresha uume iligunduliwa kwa bahati.
Simon Campbell alikuwa mkemia ambaye alikuwa akitafiti dawa ya ugonjwa wa moyo na kampuni ya Pfizer.
Aliiambia kipindi cha BBC World Service 'The Genius of Accidents' kwamba 'tuligundua dawa iitwayo amlodipine ambayo ilikuwa dawa ya nne maarufu kwa ugonjwa wa moyo.'
Wakati huo huo, Simon alifanya ugunduzi mwingine kwamba molekuli inayoitwa cyclic GMP husaidia kupumzisha misuli.
Mwanasayansi mwingine aliyehusika katika utafiti huu alisema kuwa wakati wa utafiti huu, kiungo kiligunduliwa ambacho hutumiwa kutibu shinikizo la damu ya inguinal, lakini wakati wa utafiti, timu ya Simon haikuweza kupata matokeo yaliyohitajika.
"Tulisikitishwa sana na ilionekana kana kwamba programu hiyo ingesitishwa," anaeleza.

Chanzo cha picha, Getty Images
Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.
Bonyeza hapa kujiunga
Mwisho wa Whatsapp
"Hata hivyo, uamuzi ulifanywa kwamba tungefanya jaribio la mwisho la siku kumi kwa kutumia dawa zaidi kwa watu waliojitolea kuona matokeo yake."
Ilikuwa mwanzoni mwa miaka ya 1990 wakati wanaume wa kujitolea pekee walichaguliwa kwa majaribio kama haya ya kisayansi.
“Siku kumi baada ya majaribio kumalizika, tuliuliza matokeo yake ni nini na hatukuwa na majibu mengi,” anasema Simon.
"Tuliuliza mkuu wa utafiti na alisema kuwa katika wagonjwa wa kujitolea, ambao walikuwa na ugonjwa wa moyo, maumivu ya misuli, maumivu ya kichwa na tumbo walizingatiwa."
Lakini wauguzi waliohusika katika jaribio hili pia walitoa angalizo lingine na uchunguzi huo ulikuwa kwamba watu waliojitolea walikuwa wakipata kusimama kwa uume ambao ulikuwa zaidi ya kawaida.
Kumbuka kwamba katika majaribio ya kimatibabu, watu wanaojitolea huulizwa maswali ya kawaida kama vile: Je, una maumivu yoyote? Au unajisikiaje?
Dkt. Peter Ellis pia alikuwa akifanya kazi juu ya athari za dawa hii mpya.
'Moja ya majibu tuliyopata kwa maswali haya ni kwamba watu walikuwa wakishuhudia hali isiyo ya kawaida katika uume,' anafafanua.
Matokeo haya yalikuwa ya kushangaza sana na yasiyotarajiwa kwa timu iliyohusika katika jaribio hili.
"Watu watano kati ya wanane wa kujitolea walifanya hivyo, kwa hivyo tulilazimika kujiuliza ikiwa ni athari ya muda tu ya dawa hiyo au tumegundua dawa ya ugonjwa wa kiume," anasema Dk Peter.
'Hawa watu wa kujitolea walikaa wodini kwa siku kumi na kula tulichowapa na kunywa walichoambiwa,' anasema Simon.
Dkt. David Brown, ambaye alihusika katika uvumbuzi wa Viagra, anasema bado angependa kukutana na watu hao wa kujitolea.
"Waliweka historia, ingawa wanaweza kuwa walitaka kupata pesa kidogo wakati huo, lakini walifanya mabadiliko makubwa katika maisha ya watu."

Chanzo cha picha, PFIZER
Utafiti ambao ulisababisha ugunduzi wa usiotarajiwa wa Viagra ulifanyika mnamo 1992, lakini baada ya ugunduzi huo, Pfizer ilifanya majaribio 21 zaidi.
"Majaribio haya yalihusisha wagonjwa wenye matatizo ya nguvu za kiume na katika kila jaribio dawa ilifanya kazi, ambayo ilikuwa ya kushangaza kwa sababu kwa kawaida hakuna majaribio yanayotoa matokeo 100%," anasema Simon.
Jambo jingine kuhusu majaribio haya lilikuwa la kuvutia.
Simon Campbell anasema kuwa 'kawaida mgonjwa anapopewa dawa, husahau, hakumbuki kutumia dawa hiyo', lakini katika jaribio hili hakukuwa na tatizo kama hilo.
'Niliambiwa na watu waliohusika katika jaribio hilo kwamba wagonjwa wa kujitolea walikataa kurudisha Viagra ambayo haijatumika.'
"Tulijua ni vidonge vingapi tumempa nani lakini wagonjwa walidanganya kwamba hawakuwa na vidonge zaidi."
'Sahau hizo namba, mgonjwa mwenyewe alikuwa anasema sirudishi kidonge.'
Majaribio ya kimatibabu ya Viagra yalifanikiwa sana hivi kwamba Pfizer aliamua kuileta sokoni haraka iwezekanavyo.

Chanzo cha picha, Getty Images
Ndani ya miezi sita, Mamlaka ya Dawa, FDA iliidhinisha kidonge hicho kuuzwa. Mnamo 1998, Viagra iliingia sokoni na kupata jina la 'Blue Pill'.
Kwa sababu ya watu hao wa kujitolea, mamilioni ya watu walinufaika na Viagra ikawa dawa inayotumiwa zaidi ulimwenguni.
"Jambo la kufurahisha ni kwamba wakati wa majaribio ya kwanza, athari hii ya kidonge ilipogunduliwa kwa bahati mbaya, hatukujua kuwa dawa kama hiyo ilihitajika," anasema Simon.
Lakini hili limekuwa tatizo la zamani katika historia ya dunia. Kihistoria, kutajwa rasmi kwa suala hili la kiume kunapatikana katika maandishi ya kale ya Misri ambayo yanaanzia 2,000 BC.
Madaktari wa wakati huo waliwashauri wagonjwa kupata moyo wa mamba wa mtoto na kuukanda kwenye uume, lakini ugunduzi wa Viagra ulitoa suluhisho la kimapinduzi kwa tatizo hili.
Kimsingi, Viagra inaboresha mtiririko wa damu kwa uume, Simon anaelezea.
'Ubongo wa binadamu hutoa neurotransmitter iitwayo nitriki oksidi ambayo husafiri hadi kwenye mishipa ya uume kutoa mzunguko wa GMP.'
"Watu wenye matatizo ya nguvu za kiume kwa kweli hawatengenezi kiasi cha kutosha cha GMP ya mzunguko, na Viagra inaboresha mchakato huu."
Simon anasema kwamba Viagra ni suluhu la tatizo la kiafya.
Anasema asilimia 70 ya matokeo ya vidonge vya miligramu hamsini hupatikana, lakini matokeo yake ni asilimia 60 kwa wagonjwa wa kisukari na presha, huku matokeo yakiwa ni hadi asilimia 40 kwa wagonjwa waliotolewa kibofu.
Simon anaeleza kuwa hii ni kwa sababu wakati wa kutoa kibofu, madaktari wa upasuaji hukata mishipa michache kwenye uume.
Hata hivyo, anasema kuwa ni dawa ya ufanisi. Nimejifunza kutoka kwa watu waliokuwa kwenye viti vya magurudumu kwamba sasa wanaweza kupata watoto.'
Ikumbukwe kuwa hivi sasa Viagra inatumika kutibu magonjwa mengine, huku utafiti ukifanywa ili kuweza kutibu saratani ya ubongo kwa kutumia dawa hii.















