Waziri Mkuu wa Uingereza aanza ziara yake ya kwanza nje ya nchi

Chanzo cha picha, Reuters
Waziri Mkuu wa Uingereza, Andy Burnham, anatarajiwa kuzuru Kyiv Jumatatu ya tarehe 24 Agosti 2026, katika ziara yake ya kwanza nje ya nchi tangu alipokuwa Waziri Mkuu.
Burnham anatarajiwa kuonyesha mshikamano wa Uingereza na Ukraine, huku akishiriki pia katika maadhimisho ya miaka 35 tangu Ukraine ilipopata uhuru.
Pia ataongoza kwa mara ya kwanza mkutano wa Coalition of the Willing, muungano ulioanzishwa na Uingereza na Ufaransa chini ya Waziri Mkuu wa zamani, Keir Starmer.
Burnham pia atapokea tuzo kwa niaba ya wananchi wa Uingereza, ikiwa ni kutambua mchango wa Uingereza katika kuiunga mkono Ukraine, kabla ya kushiriki katika sherehe za Siku ya Uhuru.
Ziara hiyo inafanyika wakati mashambulizi ya Urusi nchini Ukraine yakiongezeka. Ijumaa, shambulio katika kituo cha ununuzi liliripotiwa kuua watu wasiopungua 16.
Burnham amesema Ukraine ina uhakika na uungwaji mkono wa Uingereza.
Wakati huo huo, Moscow imeionya Uingereza kuhusu "madhara" yanayoweza kujitokeza kutokana na matumizi ya ndege zisizo na rubani zinazotolewa na Uingereza kwa Ukraine, ambazo Kyiv imekuwa ikitumia kushambulia miundombinu ya Urusi.





















