Hatari ya Ebola yaongezeka hadi 'juu zaidi' nchini DR Congo

Chanzo cha picha, Reuters
Kiwango cha hatari ya afya ya umma kutokana na mlipuko wa sasa wa Ebola katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo imeongezwa kutoka "juu" hadi "juu zaidi" na Shirika la Afya Duniani (WHO).
Katika taarifa mpya Ijumaa, mkuu wa WHO Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus pia alisema hatari katika eneo pana barani Afrika ilikuwa "juu", lakini imesalia "chini" duniani kote.
Aina adimu ya Ebola, inayojulikana kama Bundibugyo, haina chanjo iliyothibitishwa na inaua takriban theluthi moja ya walioambukizwa. Hadi sasa, mlipuko huo unaojikita katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo umesababisha vifo takriban 177 na visa vinavyoshukiwa 750.
Hii inakuja huku wanasayansi katika Chuo Kikuu cha Oxford nchini Uingereza wakitengeneza chanjo mpya ambayo inaweza kuwa tayari kwa majaribio ya kimatibabu ndani ya miezi miwili hadi mitatu.
Kulingana na teknolojia ile ile waliyotengeneza kwa ajili ya chanjo ya Covid ya AstraZeneca, hakuna uhakika kwamba itafanya kazi na itahitaji utafiti wa wanyama na majaribio kwa watu ili kujua kama itafanya kazi.
BBC inaelewa kuwa majaribio ya wanyama tayari yanaendelea huko Oxford.
Taasisi ya Serum ya India imepangwa kutoa chanjo ya Ebola kwa wingi mara tu Oxford itakapoweza kutoa vifaa vya kiwango cha matibabu.
Chanjo tofauti ya majaribio ya Bundibugyo pia inatengenezwa, lakini inatarajiwa kuchukua miezi sita hadi tisa kwa kipimo chochote kuwa tayari kwa majaribio.
Soma zaidi:

